TAHARIRI: Vijana wasikubali ‘Niko Kadi’ itekwe na wanasiasa
GEN Z wanastahili kujihadhari kaulimbiu yao ya ‘Niko Kadi’ isitekwe nyara na wanasiasa wanaolenga kuitumia kujivumisha wakisaka uongozi mwaka ujao.
Niko Kadi imekuwa kauli maarufu ambayo vijana wanatumia kuhimizana wajitokeze kujisajili kama wapigakura kwa ajili ya uchaguzi mkuu wa 2027.
Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka Nchini (IEBC) imetangaza kuwa kutakuwa na usajili wa wapigakura ambao utaanza Machi 30 na kuendelea kwa siku 30.
IEBC inalenga kuwasajili angalau wapigakura wapya hasa vijana ambao wamehitimu umri wa miaka 18 au wale ambao hawajajisajili miaka ya nyuma.
Wanasiasa nchini wana mazoea ya kuwaiga vijana kwa sababu sasa wanaona idadi yao kama tishio kwa nafasi zao za uongozi.
Kwa miaka mingi vijana wamekuwa wakikashifiwa kwa kujitia hamnazo kuhusu masuala ya uongozi wa nchi.
Takwimu za upigaji kura zinaonyesha vijana wengi hawajitokezi siku ya uchaguzi kupiga kura.
Hata hivyo, kwa sasa kunaonekana kuna mzinduko miongoni mwa vijana hasa baada ya maandamano ya kulalamikia Mswada wa Fedha 2024.
Tangu wakati huo, vijana wanaonekana kusisimkia masuala ya uongozi na kuwa na imani zaidi kuwa wanaweza kutekeleza mabadiliko ya utawala nchini.
Hii ndiyo inawatia hofu walio mamlakani kwa sababu vijana wakijitokeza kupiga kura, basi wanafahamu hawana lao 2027.
Kwa upande mwingine, kuna tapo la wanasiasa wa upinzani ambao wanataka kuwatumia vijana kama daraja kuingia madarakani.
Hii ni licha ya kuwa baadhi yao wamehudumu katika serikali zilizopita kwa miaka mingi na hawakujali vijana wala hawakutekeleza mabadiliko yoyote ya uongozi.
Viongozi hawa ni sawa tu na wale waliopo mamlakani kwa sababu wanalenga kuwatumia vijana kuchukua mamlaka.
Katika tapo la wanasiasa wa sasa, hakuna mrengo ambao unaweza kusema umewahi kuwa na suluhu kwa changamoto za vijana.
Wamewaajiri vijana wangapi? Wamezima ukatili dhidi ya vijana kivipi? Wengi wao wamekuwa tu wakiwatumia vijana kuendeleza maasi nchini kisha kuwalipa mapeni machache.
Kwa hivyo, serikali, upinzani na Linda Mwananchi wote wanataka tu kudandia Niko Kadi kwa manufaa yao wala si kuwasaidia vijana.
Hii ndiyo maana vijana lazima wawe makini, waangalie malengo yao na kutumia idadi yao kwa hekima kuamua uongozi wa nchi.