Familia yasaka haki kufuatia kuuawa kwa mwanamke aliyeenda sherehe za Idd-ul-Fitr
FAMILIA ya mwanamke aliyepatikana ameuawa Likoni wikendi, imetaka polisi iharakishe uchunguzi na kukamata waliohusika kwa uhalifu huo.
Mnamo Machi 18, Elizabeth Nina aliondoka nyumbani kwake Likoni, akielekea kusherehekea Idd-ul-Fitr, ambayo ilikuwa imepangwa kufanyika Machi 20, nyumbani kwa rafiki yake wa karibu.
Hata hivyo, mwili wake ulipatikana siku nne baadaye, ukiwa umetupwa katika jengo ambalo halijakamilika katika eneo hilo hilo.
Dada yake, Bi Everlyn Kamene, alisema Elizabeth, 34, ambaye alikuwa na ujauzito wa miezi mitano, hakuonyesha dalili zozote za kutatizika alipoondoka nyumbani.
Rafiki yake, Bi Kishindo Bamama, alisema walikuwa pamoja Ijumaa jioni katika sehemu yao ya kawaida ya burudani.
“Alitusalimia, kisha kijana mmoja akaja na kumnong’onezea jambo,” alisema.
Wakati huo, wawili hao waliondoka kwa njia tofauti, na ilikuwa mara yake ya mwisho kumwona hai.
Kamanda wa polisi wa Kaunti-ndogo ya Likoni Joseph Mutungi, alisema tukio hilo liliripotiwa na mzee wa kijiji.
Baada ya hapo maafisa walifika eneo la tukio na kuukuta mwili ukiwa umetupwa kwenye rundo la taka ndani ya jengo lililoachwa karibu na Losa Joy Academy.
Alisema uchunguzi wa awali wa mwili ulibaini kuwa ulikuwa na michubuko usoni na uvimbe kwenye sikio la kulia.
Kulingana na Bw Mutungi, inaaminika mauaji hayo yalifanyika sehemu nyingine kabla ya mwili kutupwa katika eneo hilo.
Mbunge wa Likoni, Mishi Mboko, amelaani mauaji hayo, akiyataja kuwa sehemu ya mwenendo wa kutisha wa ukatili dhidi ya wanawake katika eneo hilo.
Katika taarifa, Bi Mboko alisema alishtushwa sana na kifo cha Nina, akibainisha kuwa hakuna familia inayopaswa kupitia maumivu ya aina hiyo.
Tukio hilo linajiri wiki moja tu baada ya mwili wa msichana mwenye umri wa miaka 11 aliyekuwa amepotea kupatikana ukiwa umewekwa ndani ya mfuko katika eneo la Mjambere, Kaunti Ndogo ya Kisauni.
Msichana huyo, Glorious Kaiza, alikuwa akicheza nje na marafiki zake na ghafla akatoweka.
Makundi ya haki za binadamu Mombasa yamelaani mauaji ya hivi karibuni, yakionya kuwa yanaashiria ongezeko la kutisha la ukatili wa kijinsia unaowalenga wanawake na wasichana katika kaunti hiyo.