IEBC kuwasajili wapiga kura 2.5 milioni baadhi ya walengwa wakiwa vijana
TUME Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) imepanga kutuma wafanyakazi 12,000 katika vituo zaidi ya 30,000 wakati itapoanzisha zoezi la Taifa la Usajili Endelevu wa Wapigaji Kura (ECVR) Jumatatu, Machi 30, 2026, ikilenga kusajili wapiga kura wapya 2.5 milioni.
Akizungumza jijini Nairobi wakati wa hafla ya kutia saini Makubaliano (MoU) kati ya IEBC na Kenya Media Sector Working Group (KMSWG), Mwenyekiti wa IEBC, Erastus Ethekon, alisema kuwa wanakabiliwa na kazi kubwa, ikiwemo usimamizi wa Uchaguzi Mkuu za 2027.
“Tunakabiliwa na kazi kubwa mbele yetu, ya kwanza ni Usajili Endelevu wa Wapigaji utakaozinduliwa Machi 30, 2026. Tumewaandaa wafanyakazi 12,000 watakaonza kazi Jumatatu, Machi 30, katika vituo zaidi ya 30,000 kote nchini kwa zoezi hili,” alisema.
Kulingana na Bw Ethekon, kutokana na mafunzo waliyopata kutoka zoezi la Usajili Endelevu wa Wapigaji (CVR), ECVR imeundwa kushughulikia mapungufu ya kiufundi na kiutendakazi, ikiwemo kupeleka huduma karibu na wananchi, kuwafikia vijana, na usambazaji wa rasilimali kwa kuzingatia data.
“Tunakusudia kuwasajili wapiga kura wapya takriban 2.5 milioni wakati wa zoezi hili, ” aliongeza.
Akizungumza katika hafla hiyo hiyo, Rais wa Chama cha Wahariri Kenya (KEG), Zubeida Kananu, alisema Kenya inaimarisha maandalizi ya uchaguzi ujao, ikionyesha umuhimu wa wadau wa kimataifa katika kuimarisha demokrasia.
“Kama nchi inavyoanzia kujipanga mapema badala ya kukabiliana na dharura za mwisho, sasa kipaumbele ni usajili wa wapiga kura,” alisema.
“Mnamo 2022, tulikuwa tukishughulikia dharura kwa haraka, tukitia saini makubaliano dakika za mwisho. Leo hatusubiri dakika za mwisho; tunapanga mapema.”
Kwa upande wake, Katibu wa chama cha Wanahabari Kenya (KUJ), Eric Oduor, alisema makubaliano hayo ni ya kurahisisha ushirikiano kati ya vyombo vya habari na IEBC na haitaharibu kazi za pande zote.
“MoU hii ni suluhisho la baadhi ya changamoto zilizojitokeza katika uchaguzi wa awali, kama vile upatikanaji wa taarifa.”
, kwani umma huwa na hofu wakati taarifa hazipatikani. Tunataka kuona wagombea wanaochochea ghasia wakichukuliwa hatua ili waandishi na wananchi wahisi kuwa salama,” alisema.
Oduor alisema ushirikiano huo utasaidia vyombo vya habari kutoa taarifa kwa wakati muafaka na zisizo na shaka kwa wananchi.