Habari

Ichung’wah akatiza hotuba yake baada ya kuzomewa Kiambu mbele ya Ruto

Na SIMON CIRU March 28th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

ZIARA ya maendeleo ya Rais William Ruto  Kaunti ya Kiambu iliyokusudiwa kuwa jukwaa la kuvutia wapigakura kabla ya Uchaguzi Mkuu wa 2027, iligeuka mkutano wa kisiasa wenye hisia huku washirika wakuu wa rais wakikabiliwa na upinzani mkali kutoka kwa umma.
Mshirika wa karibu wa rais, Kimani Ichung’wah, ambaye ni Mbunge wa Kikuyu na Kiongozi wa Wengi katika Bunge la Kitaifa, alizomewa vikali katika Uwanja wa Thika na kulazimika kukatiza hotuba yake kutokana na kelele.
Ichung’wah alimweleza Rais kuwa waliokuwa wakimzomea ni sehemu ya kundi linalopinga maendeleo Kiambu, akidai kuwa wanapotosha wananchi kwa kusema miradi inayopangwa ni njama ya kunyakua ardhi ya umma.
Hata hivyo, katika majibu ya haraka, Gavana wa Kiambu Kimani Wamatangi alikanusha madai hayo akisema hajawahi kupinga miradi ya serikali kwani inalenga kuwafaidi wananchi.
“Sipingi maendeleo yoyote. Msikubali kudanganywa,” alisema Wamatangi.
Rais Ruto, aliyeonekana kukerwa na hali ya uhasama na mivutano hadharani kati ya viongozi wa chama chake cha United Democratic Alliance (UDA), alisema hakuna mtu mwenye uwezo wa kuzuia maendeleo, akisisitiza kuwa yeye ndiye Rais wa Kenya.
Alikiri kuwa kuna ushindani mkali wa kisiasa Kiambu lakini hakutoa maelezo ya kina.
“Ninaona kuna ushindani mkali Kiambu. Hakuna mtu anaweza kuzuia maendeleo kwa sababu ni haki ya wananchi na mimi ndiye Rais,” alisema.
Hata hivyo, mvutano uliendelea washirika wengine wa rais waliposimama kuzungumza. Mbunge wa Thika Town Alice Ng’ang’a, ambaye ametangaza nia ya kuwania ugavana wa Kiambu, pia alizomewa. Wawakilishi wa wanawake wa Kiambu Ann Wamuratha na Murang’a Betty Maina nao hawakusazwa.
Katika eneobunge la Juja, ambako Rais alizindua mradi wa makazi nafuu wa Nyacaba akiwa mwenyeji wa Mbunge George Koimburi, mbunge huyo aliwaambia wakazi kuwa aliamua kumuunga mkono Ruto ili kumsaidia kupata muhula wa pili katika uchaguzi ujao wa urais.
Akiwa Thika mjini, ambapo alizindua ujenzi na upanuzi wa uwanja wa michezo wa Thika utakaogharimu Sh900 milioni, Rais alikosoa wapinzani wake kisiasa. Bila kutaja majina, alisema wanaoshutumu serikali kwa ufisadi ndio wahusika wakuu wa wizi, akirejelea sakata ya ardhi ya Ruaraka.
“Hao ndio wezi wakubwa. Waliiba ardhi ya Ruaraka na sitaruhusu wapotoshe wananchi kwa siasa za ukabila,” alisema Ruto.
Aliongeza kuwa uwanja huo mpya utakuwa na uwezo wa kuketi watu 10,000 na utakamilika kufikia Desemba mwaka huu, akisema ni uwekezaji muhimu utakaokuza vipaji vya michezo.
Kaunti ya Kiambu imeendelea kuwa ngome muhimu kisiasa tangu uchaguzi wa 2022 ambapo Rais Ruto na aliyekuwa naibu wake Rigathi Gachagua walipata takriban kura milioni 1.3 za urais.
Tangu wakati huo, Kiambu imekuwa uwanja wa ushindani mkali wa kisiasa huku wagombea wakijaribu kujenga miungano imara kuvutia kura nyingi.