Habari

Aliyekata rufaa akipinga hukumu ya miaka 14 jela ahukumiwa kifo

Na JOSEPH WANGUI March 29th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

WAKATI Daniel Njihia Miano alipokata rufaa kupinga kifungo chake cha miaka 14 jela, alitarajia kupata nafuu na fursa ya kurejea kwa familia yake.

Badala yake, Mahakama ya Rufaa wiki iliyopita ilithibitisha uamuzi wa awali uliompa adhabu ya kifo, ikiangazia hatari ya kukata rufaa katika kesi za jinai.

Kama asingekata rufaa, Miano angekuwa huru leo, baada ya kuhukumiwa kifungo cha miaka 14 Desemba 2010. Hata hivyo, Mahakama Kuu iliongeza adhabu hiyo hadi kifo katika uamuzi wa Oktoba 2012.

Mahakama ya Rufaa ilitupilia mbali rufaa yake ya pili, ikithibitisha uamuzi wa Mahakama Kuu.

Miano alishtakiwa kwa kosa la wizi wa kutumia nguvu kufuatia shambulio la Septemba 2010 katika Kaunti ya Nyandarua, ambapo Philip Karuoya Wambugu aliibiwa Sh2,100 na simu mbili za mkononi za thamani ya jumla ya Sh6,750.

Tukio hilo lilitokea katika kijiji cha Ritaya, ambapo washambuliaji waliokuwa na mapanga na rungu walimvamia mlalamishi.

Upande wa mashtaka uliwasilisha mashahidi watano, akiwemo mlalamishi, huku Miano akikanusha mashtaka hayo na kutoa utetezi wake bila kiapo.

Mahakama ya kwanza ilimpata na hatia ya wizi wa kawaida na kumpa kifungo cha miaka 14. Hata hivyo, Miano hakuridhika na akakata rufaa kupinga hukumu na adhabu, huku upande wa mashtaka ukiwasilisha notisi ya kutaka adhabu iongezwe.

Kesi ilipofika Mahakama Kuu, majaji walimuonya kuhusu hatari ya kuendelea na rufaa hiyo, lakini alichagua kusonga mbele.

Mahakama Kuu ilikubaliana na upande wa mashtaka, ikisema ushahidi ulithibitisha kosa la wizi wa kutumia nguvu na hivyo kubadilisha kifungo cha miaka 14 kuwa adhabu ya kifo.

Bado hakuridhika na akaenda Mahakama ya Rufaa. Mawakili wake walidai kuwa Mahakama Kuu ilikosea kuongeza adhabu bila kufuta rasmi hukumu ya awali ya wizi wa kawaida.

Hata hivyo, Mahakama ya Rufaa ilikataa hoja hiyo, ikisema mahakama ya rufaa ina mamlaka ya kudumisha hatia huku ikibadilisha adhabu, mradi mshtakiwa alipewa onyo la haki.

Majaji walibainisha kuwa Miano alifahamishwa wazi hatari hiyo lakini akaamua kuendelea. Uamuzi huo ulimgharimu pakubwa.

Mahakama ilisema ushahidi ulionyesha kuwa alishirikiana na wengine katika uhalifu huo, jambo muhimu katika kosa la wizi wa kutumia nguvu.

Hatimaye, rufaa ilitupiliwa mbali kwa kukosa mashiko, korti ikisisitiza kuwa rufaa za jinai zinaweza kugeuka na kuwa na matokeo mabaya zaidi kwa mshtakiwa.