Habari za Kitaifa

Wakazi wa Ol Kalou wapigwa na butwaa kubaini mbunge Kiaraho alikataa kuzikwa kwao

Na WAIKWA MAINA April 1st, 2026 Kusoma ni dakika: 2

WAKAZI wa Ol Kalou wamepigwa na butwaa kufuatia uamuzi wa mbunge wao marehemu David Njuguna Kiaraho kutaka azikwe nje ya eneo bunge hilo.

Kwa wengi, uamuzi huo wa mwisho unaangazia urithi tata wa mwanasiasa aliyekuwa na mienendo isiyotabirika akiwa hai na sasa hata baada ya kifo chake.

Kama ilivyokuwa kawaida yake katika siasa, matakwa yake ya mwisho yameibua mjadala mkubwa katika jamii aliyowakilisha tangu 2013.

Eneo atakalozikwa katika makazi yake ya Tigoni, Limuru, Kaunti ya Kiambu, lilithibitishwa Jumatatu jioni na kamati andalizi ya mazishi inayoongozwa na Mbunge wa Kinangop Kwenya Thuku na msaidizi wake- Mwakilishi wa Wanawake wa Nyandarua Faith Gitau.

Katika tangazo hilo, waliweka wazi kuwa mazishi yatafanyika nje ya kaunti aliyohudumia kwa muda mrefu.

Maandalizi tayari yameanza katika eneo la Ol Kalou huku viongozi na wakazi wakijipanga kumpa heshima za mwisho.

“Familia ya marehemu, kwa mashauriano na kamati ya mazishi, imetangaza Ijumaa, Aprili 10, 2026 kuwa siku ya mazishi. Ibada ya mazishi itafanyika katika Kanisa la St Andrew’s, Nairobi, kisha mwili uzikwe katika shamba lake la Tigoni, Limuru, kulingana na matakwa yake ya mwisho,” alisema Bw Thuku kwa niaba ya familia na kamati.

Kwa mujibu wa ratiba, mkesha utafanyika Aprili 6 nyumbani kwake kijijini Munyeki, kabla ya ibada ya wafu kufanyika katika Uwanja wa Ol Kalou Aprili 7.

Familia itatumia wikendi ya Pasaka nyumbani kwao Ol Kalou kabla ya mazishi kufanyika Kiambu.

Kamati za mazishi zimekuwa zikikutana katika afisi za NG-CDF Ol Kalou lakini zinatarajiwa kuhamia nyumbani kwa marehemu siku zinavyosonga.

Hata hivyo, uamuzi wa kuzikwa Tigoni umeibua hisia kali miongoni mwa wakazi wa Ol Kalou, wengi wakihisi mbunge huyo angefaa kuzikwa katika eneo alilohudumia kisiasa.

Mzee Isaac Ngugi alisema ni jambo la kusikitisha kuona kiongozi aliyewahudumia kwa miaka mingi hakutaka kuzikwa miongoni mwa watu waliokuwa wakimchagua.

“Wengi wetu hatukuzaliwa Nyandarua lakini tulijitolea kuihudumia. Inasikitisha kuwa moyo wake ulibaki Tigoni,” alisema.

Mfanyabiashara John Githinji alisema ingawa Kiaraho alijulikana kwa maamuzi ya kushtua, hatua hiyo ilikuwa ya kushangaza zaidi.

“Tulijua ana tabia ya kushtua watu, lakini hii imevuka matarajio. Wakati wa kampeni wapinzani wake walimuita mgeni, na sasa inaonekana alikuwa na uhusiano mkubwa zaidi na Limuru,” alisema.

Baadhi ya wakazi wamechukulia uamuzi huo kama funzo muhimu kwao kuchagua viongozi wenye mizizi katika maeneo wanayogombea.

Bw Mwangi Samuel alisema Nyandarua inahitaji viongozi wanaotoka eneo hilo ili kuleta maendeleo ya kweli.

Hata hivyo, MCA maalumu Stephen Mureithi, ambaye alikuwa mshirika wa karibu wa marehemu aliwataka wakazi kuheshimu matakwa yake ya mwisho.

Alisema uongozi wa Kiaraho ulijikita katika maendeleo na ulitambuliwa kitaifa kupitia utekelezaji bora wa miradi ya NG-CDF.

Maisha ya kisiasa ya Kiaraho yalijulikana kwa kutotabirika. Katika uchaguzi wa 2017, alifanya mabadiliko ya ghafla na kushinda licha ya kuonekana kwamba alikuwa amekubali kushindwa na mpinzani wake mkuu Kanuri Wambugu.

Katika uchaguzi wa 2022, aliwaacha wafuasi wake wakikisia kuhusu chama cha kutumia hadi dakika za mwisho alipothibitisha kuwania kiti chake kwa tiketi ya Jubilee.

Hata wakati wa mchakato wa kumng’oa aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua, alikwepa kikao cha Bunge siku ya kupiga kura kabla ya kuunga mkono upande wa UDA katika dakika za mwisho.

Mchambuzi wa siasa John Kariuki alisema nguvu za Kiaraho zilikuwa katika mtandao wake wa “Kiaraho Mashinani” na kundi lake la karibu lililojulikana kama “Pentagon.”

Hata hivyo, alibainisha kuwa udhaifu wake ulikuwa kujaribu kufurahisha kila mtu kisiasa.

“Wengi wanaamini pesa zilimjenga kisiasa, lakini ukweli ni kwamba yeye ndiye aliyedhibiti pesa, si pesa kumdhibiti,” alisema Kariuki.