Dondoo

Jombi akwama kwenye kaburi alikoenda kutekeleza uchawi

Na KALUME KAZUNGU April 1st, 2026 Kusoma ni dakika: 1

MARIKEBUNI, Kilifi

JOMBI aliyeshukiwa kwa ushirikina eneo hili aliaibika alipojipata amekwama juu ya kaburi alikoenda kutekeleza uchawi.

Inaaminika boma hilo lilizindikwa au kuwekwa fingo kuzuia wachawi waliosheheni mitaani wasilinyemelee.

Kwa miaka mingi, wenye boma hilo wamekuwa wakipoteza watu wao kupitia nguvu za uchawi.

Waliosalia pia walikuwa hawapati amani, hasa usiku, hivyo wakaafikia kutafuta waganga wa kienyeji ili kulizindika.

Hata hivyo, kujiamini kwa jombi huyo ambaye amekuwa akihangaisha na kusumbua wengi mtaani hapa kulifikia ukingoni baada ya kujikuta amekwama kimiujiza juu ya kaburi huku akiwa uchi wa mnyama.

Isitoshe, alijipata akienjoi kula kinyesi alichokuwa amekitoa juu ya kaburi hilo.

Wenye boma walipoamka asubuhi na mapema walishangaa kumpata jamaa akiwa juu ya kaburi hilo huku akipiga gumzo peke yake.

Ni hali iliyovutia umati mkubwa, ikiwemo wenyeji na majirani huku wazee wa mtaa wakiitwa kushughulikia hatima ya jombi huyo aliyenaswa na fingo.