Habari

Kampuni kumlipa mfanyakazi aliyenyanyaswa na bosi wake Sh1.3m

Na JOSEPH WANGUI April 4th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MKURUGENZI Mkuu wa kampuni moja ya teknolojia jijini Nairobi amepatikana na hatia ya unyanyasaji wa kijinsia dhidi ya mfanyakazi wake wa chini, baada ya mahakama kubaini kuwa ujumbe wake wa WhatsApp ulikuwa na maudhui ya kingono na kuvuka mipaka ya kikazi.

Kwa mujibu wa kesi hiyo, mkurugenzi huyo, aliyetambuliwa kama OL, alikuwa akimtumia mfanyakazi huyo wa idara ya fedha, RA, ujumbe na vibonzo vilivyokuwa na ishara za kingono.

Ingawa mwanzoni mawasiliano hayo yalionekana ya kawaida, yalizidi kumkera mfanyakazi huyo kutokana na nafasi ya bosi wake kama msimamizi wake wa moja kwa moja.

Mahakama ilielezwa kuwa mnamo Septemba 2022, mkurugenzi huyo alimtumia ujumbe uliokuwa na maana fiche za kingono pamoja na video ya TikTok ya wimbo wa ohangla uliokuwa na maneno ya kuchochea hisia.

Hali hiyo iliendelea hata mwaka uliofuata, licha ya mfanyakazi huyo kudumisha uhusiano wa kikazi.

Mnamo Januari 2023, hali ilichukua mkondo mpya baada ya mkurugenzi huyo kumkosoa mfanyakazi huyo kuhusu utendaji wake, kabla ya kumbusu bila idhini alipokuwa akimpeleka nyumbani.

Siku chache baadaye, mfanyakazi huyo alidai alishambuliwa kingono ndani ya gari la bosi wake baada ya hafla ya kikazi.

Mfanyakazi huyo aliambia mahakama kuwa tukio hilo lilimwacha katika hali ya huzuni na mshtuko mkubwa, na alilazimika kutafuta matibabu.

Shahidi mmoja alithibitisha kuwa alimkuta akilia na kushtuka.

Hata hivyo, mkurugenzi huyo alikanusha madai hayo akisema kuwa mfanyakazi huyo ndiye aliyekuwa na tabia isiyofaa, akidai alikuwa amelewa na alionyesha ishara za kimapenzi kwake.

Licha ya madai hayo, mahakama ilibaini kuwa ujumbe wa WhatsApp uliotumwa ulikuwa wa unyanyasaji wa kijinsia.

Jaji alisisitiza kuwa kutumia vichekesho au lugha ya mzaha hakuhalalishi kusambaza maudhui ya kingono kwa mfanyakazi wa chini.

Mahakama pia ilitupilia mbali hoja kuwa majibu ya mfanyakazi huyo kwa kutumia alama za tabasamu yalihalalisha vitendo vya mkurugenzi huyo.

Aidha, mahakama ilibaini kuwa mazingira ya kazi yalikuwa a ya uhasama na yasiyovumilika, hali iliyomlazimu mfanyakazi huyo kujiuzulu.

Kwa msingi huo, mahakama iliamua kuwa mfanyakazi huyo alifukuzwa kazi kwa njia isiyo ya moja kwa na kumpa fidia ya mshahara wa mwezi mmoja pamoja na mishahara ya miezi kumi, jumla ya Sh1.32 milioni.

Mahakama pia ilikataa madai ya kampuni hiyo iliyomtaka mfanyakazi huyo alipe Sh6.6 milioni kwa kuondoka kazi bila notisi.

Uamuzi huo umeangazia wajibu wa waajiri kuhakikisha mazingira salama ya kazi na kushughulikia malalamishi ya wafanyakazi kwa haki na uwazi.