Makala

Sababu ya idara kuonya wakulima kuhusu mvua

Na BENSON MATHEKA April 5th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

Idara ya Hali ya Hewa nchini Kenya imetoa onyo kwa wakulima kwamba mvua ya Aprili itakuwa chache sana mwanzoni mwa mwezi kabla ya kuimarika baadaye.

Kulingana na idara hiyo, wakulima kote nchini wako katika hatari ya kupoteza mazao yao iwapo watapanda mapema sana mwezi huu.

Idara hiyo imeonya kuwa mvua ya Aprili itapungua kwa kiasi kikubwa katika wiki mbili za kwanza kabla ya kuongezeka kadri mwezi unavyoendelea.

“Aprili 2026 inatarajiwa kuwa kilele cha msimu wa mvua za masika, ingawa mvua itakuwa chini ya wastani katika nusu ya kwanza ya mwezi na kuongezeka kuelekea mwisho,” idara ilisema.

Tahadhari hiyo imo katika Jarida la Kila Mwezi la Kilimo na Hali ya Hewa la Aprili 2026, lililotolewa Aprili 4, ambalo linaonyesha taswira mseto ya msimu wa mvua ya masika na kueleza matarajio ya wakulima kote nchini mwezi huu.

Kutokana na jarida hilo, mvua ya karibu na wastani inatarajiwa kunyesha katika kaunti za Nyeri, Kirinyaga, Murang’a, Nyandarua, Kiambu, Meru, Embu, Tharaka Nithi, Nairobi, Laikipia, Busia, Migori, Kisumu, Siaya na Homa Bay, hali itakayotoa matumaini ya uzalishaji mzuri katika maeneo yenye uwezo mkubwa wa kilimo pindi mvua itakapoimarika.

Aidha, unyevu wa udongo unatarajiwa kuwa wa wastani mwanzoni mwa Aprili lakini utaongezeka taratibu kadri mvua itakavyozidi kuelekea mwisho wa mwezi. Viwango vya juu vya unyevu katika Nyanda za Juu, Bonde la Ziwa Victoria na Bonde la Ufa pia vinaweza kusababisha maji kusimama mashambani.

Kaunti za Machakos, Kitui, Makueni, Kajiado, Taita-Taveta, Mombasa, Kwale, Kilifi, Tana River na Lamu zinakabiliwa na changamoto tofauti. Unyevu mdogo wa udongo na msongo maeneo fulani unatarajiwa, hali inayofanya uvunaji na uhifadhi wa maji kuwa muhimu ili kuhakikisha mazao yanadumu.

Wakulima katika maeneo yenye mvua nyingi wanashauriwa kuimarisha mifumo ya mifereji ya maji sasa kabla ya mvua kubwa kuanza. Kusimama kwa maji na kuharibika kwa mizizi ni hatari halisi katika Nyanda za Juu na Bonde la Ziwa Victoria kadri mvua za mwisho wa mwezi zitakavyozidi.

Shinikizo la wadudu na magonjwa ya mimea pia linaongezeka. Idara hiyo imeonya kuwa ongezeko la unyevunyevu linaweza kusababisha milipuko ya wadudu waharibifu na magonjwa ya kuvu, ikiwataka wakulima kukagua mashamba yao mara kwa mara na kuchukua hatua mapema pindi dalili zinapoonekana.

“Wakulima wanapaswa kupanga upanzi kulingana na kuimarika kwa mvua, kupalilia mazao, kuhakikisha mitaro mizuri katika maeneo yenye mvua nyingi na kuhifadhi maji katika maeneo kame,” ilishauri idara.

Maeneo yaliyokumbwa na mafuriko mwezi Machi yako katika tahadhari kubwa, huku idara ikionya wazi kuwa mafuriko yanaweza kujirudia mvua kubwa za mwishoni mwa Aprili zitakapoanza.

“Kuna pia haja ya kuwa macho dhidi ya dhoruba, mafuriko, na milipuko ya wadudu au magonjwa, na kutumia taarifa za mara kwa mara za hali ya hewa kuongoza shughuli za kilimo,”idara ilisisitiza.

Kenya Met inawahimiza wakulima wote, bila kujali eneo, kutegemea utabiri wa muda mfupi wa hali ya hewa ili kuongoza maamuzi ya kila siku ya kilimo huku nchi ikiingia katika msimu wa mvua za masika unaotarajiwa kuwa usiotabirika lakini wenye athari kubwa.