Mkaguzi aanika hali mbaya kwenye magereza licha ya mageuzi ya Awori
RIPOTI ya Mkaguzi wa Hesabu za Serikali Nancy Gathungu imeanika hali mbaya ya magereza nchini hali inayodidimiza mageuzi makubwa yaliyoanzishwa na Makamu wa Rais wa zamani Moody Awori.
Maswali sasa yameibuka kunakoelekea mabilioni ya pesa ambayo serikali huwa inatengea Idara ya Urekebishaji tabia.
Magereza mengi bado yana paa ambazo zina mabati yaliyochakaa na yamezeeka.
Kwenye baadhi ya magereza, wafanyakazi huwa wanaishi kwenye nyumba ambazo zipo katika hali mbaya.
Mwaka huu wa kifedha wa 2025/26 Idara ya Huduma za Urekebishaji tabia ilitengewa Sh38.15 bilioni ikilinganishwa na Sh34.39 bilioni mwaka wa kifedha wa 2024/25.
Kando na msongamano wa mahabusu, magereza mengi hayana ukuta na dari nzuri kwa wafungwa wa makosa makubwa wanaotumikia vifungo vya kipindi kirefu.
Pia hazina camera za CCTV, paa ambazo zinavuja, wafungwa hula vyakula vilivyopikwa vibaya huku maisha gerezani yakiwasononesha sio mahabusu tu bali pia wafanyakazi.
Hali mbaya kwenye magereza imenakiliwa katika ripoti ya ukaguzi wa idara hiyo 2024/25.
Ukaguzi huo ulifuatia kutembelewa kwa magereza 23 kati ya Julai na Agosti 2025.
Hali hiyo mbaya inaendea kinyume cha Sheria ya Makazi, Usalama na Afya ya 2007 iliyopitishwa kuhakikisha magereza yapo katika hali nzuri kwa wafungwa.
“Ni wazi kuwa Idara ya Huduma za Urekebishaji imekiuka sheria katika kutekeleza wajibu wake. Hii ni kwa sababu miundomsingi na majengo yako katika hali mbaya,” ikasema ripoti hiyo ya ukaguzi.
Kwa mfano katika Gereza la Nanyuki, hakuna dari kwa wafungwa hatari jambo ambalo ni tishio kuu la kiusalama.
“Nyumba ambako mahabusu huishi zinahitaji kutengenezwa sakafu na pia vyoo vinahitaji kukarabatiwa. Nyumba za wafanyakazi nazo zinahitaji kufanyiwa ukarabati na kupakwa rangi,” ikasema sehemu ya ripoti hiyo ya mkaguzi.
Kwenye Gereza la Meru, nyumba 10 zinahitaji paa mpya, mbao na pia mabati mapya. Nyumba 90 za wafanyakazi nazo zinahitaji kukarabatiwa na pia kuimarishwa kwa miundomsingi nyingine.