Habari

Wandayi, Lee kuchunguzwa kuhusu sakata ya mafuta

Na ERIC MATARA April 6th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MAWAZIRI wawili ni kati ya wanaochunguzwa kuhusu sakata ya mafuta ya Sh4.8 bilioni ambayo imesababisha kukamatwa na kujiuzulu kwa wakuu watatu wa sekta ya kawi.
Sakata hiyo inahusisha kuingizwa kwa shehena mbili zilizobeba petroli ya tani 128,000 nje ya makubaliano ya kiserikali maarufu kama G to G. Chini ya makubaliano hayo, serikali ina wajibu wa kununua mafuta kutoka Saudi Arabia na Mmilki ya Kiarabu.
Jana, barua mbili zinazohusishwa kuingizwa kwa mafuta hayo zilifichuliwa na kumhusisha Waziri wa Kawi Opiyo Wandayi na mwenzake wa Biashara Lee Kinyanjui.
Wawili hao sasa wanatakiwa kuandikisha taarifa na Mkurugenzi wa Idara ya Upelelezi Nchini (DCI) kutoa maelezo kuhusu kile wanachokijua kuhusu sakati hiyo ambayo imetokea baada ya Kampuni ya Mafuta nchini (KPC) kubinafsishwa kwa kima cha Sh106 bilioni.
Jana, Rais Ruto alionya kuwa serikali itapambana na wakora ambao wanajaribu kutumia uhaba wa mafuta unaotokana na vita Mashariki ya Kati kuwaibia Wakenya.
Barua ambazo Taifa Leo imeona inahusishwa na kuidhinishwa kwa kuingizwa kwa mafuta hayo nchini na mwongozo ambao ulifuatwa.
 “Mawaziri hao watahitajika kutoa maelezo kuhusu kuingizwa kwa mafuta hayo wala hili si suala la maafisa wadogo pekee. Lazima tumakinikie uamuzi uliofanywa na wakuu na stakabadhi hizo zitakuwa na umuhimu,” akafichua afisa mmoja wa ngazi ya juu katika Idara ya Upelelezi Nchini (DCI).
Kwenye mojawapo ya barua hiyo Bw Kinyanjui amemwandikia Bw Wandayi akitaka ushuru uondolewe kwa bidhaa za petroli.
 “Kuhusiana na barua kutoka Idara ya Petroli Machi 26 na Machi 27, 2028, ushuru umeondolewa kwa petroli ambayo ina madini ya juu ya Manganese, Sulphur na Benzene,” ikasema sehemu ya barua hiyo.
Kwenye mahojiano jana, Bw Kinyanjui alijitenga na sakata hiyo ya mafuta, akisema barua alizoandika zilikuwa za kutoa masharti ya kutimizwa kwa sababu uagizaji wa mafuta ungeathirika.
“Sifahamu mengine kando na barua ya uidhinishaji na nilifanya tu kile ambacho sheria inahitaji nifanye. Nilikuwa nasisitiza tu kuwa iwapo hili lazima lifanyike basi lazima mtimize masharti,” akasema Bw Kinyanjui. Alisisitiza barua yake pia iliamrisha Shirika la Kukadiria Ubora wa Bidhaa (KEBS) lishirikishwe.
Alifichua pia kuwa hakujibiwa na Wizara ya Kawi baada ya kuidhinisha ushuru uondolewe mafuta yaliyokuwa yakiagizwa.
Bw Wandayi jana hakuwa amejibu ujumbe aliotumiwa na Taifa Leo hasa kuhusu barua ambayo alikuwa ameandikiwa na Bw Kinyanjui.
Baadaye alituma taarifa akisema serikali itapambana na mawakala na wakora ambao wanatumia vita vya mashariki ya kati kusababisha uhaba wa petroli kwa lengo la kuwafilisi Wakenya