Kimataifa

Iran yasema ingali inadhibiti Hormuz licha ya kunyeshewa mabomu na Amerika wiki 2 mfululizo

Na MASHIRIKA July 28th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

DUBAI, UAE:

IRAN imesema ingali inadhibiti Mkondo-Bahari wa Hormuz wala haikusudii kurejelea mazungumzo ya amani na Amerika baada ya Rais Donald Trump kusitisha kampeni ya mabomu ya wiki mbili ambayo wandani wake walimweleza imetimiza malengo yake.

Kufuatia mashambulizi makali ya mabomu siku 13 mfululizo yaliyosababisha Tehran kulenga ngome za Amerika kulipiza kisasa, Trump alisimamisha kampeni hiyo wikendi.

Iran ilisema itasitisha mashambulizi yake binafsi kwa kipindi ambacho Amerika itasimamisha.

Mwisho wa kampeni ya mabomu ya Amerika ulisababisha bei za mafuta kushuka kwa matumaini kuwa michakato ya usambazaji bidhaa iliyotatizwa duniani itarejelea shughuli zake.

Lakini kwa ishara kuwa Tehran huenda tayari inafanyia majaribio mkataba mpya wa kusitisha vita, Jordan iliripoti kuangusha droni mbili na duru za usalama za Iraq zikasema droni hizo zililenga wapiganaji wa Wakurdi wa Iran eneo la Iraq Kaskazini.

Majeruhi hawakuripotiwa katika visa hivyo.

Uamuzi wa Trump kusitisha kampeni unaashiria ushauri kutoka kwa jeshi lake kwamba mabomu, yaliyonuiwa kuvunja udhibiti wa Irani kwenye mkondo, yamefikia upeo ambao yangeweza kufanikisha, kulingana na afisa wa Amerika na ripoti kadhaa za vyomvo vya habari.

Afisa wa Amerika alisema kwamba makamanda wa jeshi walimshauri rais kwamba wameishiwa na vituo vya kushambulia.

Mwenyekiti wa Wakuu wa Wahudumu, Jenerali Dan Caine, alielezea wasiwasi kuhusu kumalizika kwa silaha za kujikinga angani, alisema afisa.

Balozi wa Amerika katika Umoja wa Mataifa, Mike Waltz, alisema Jumapili kuwa Trump alisitisha kampeni kuruhusu majadiliano.

Trump, Waziri wa Masuala ya Kigeni Marco Rubio na maafisa wengine wa Amerika wameelezea Iran kama “inayosihi kuwepo mkataba.”

Lakini msemaji wa Wizara ya Masuala ya Kigeni Iran, Esmail Baghaei, alisema katika kikao cha vyombo vya habari jana kwamba Iran haijaomba kurejelea mazungumzo ya amani na Amerika.

Jumbe bado zilitumwa kati ya pande husika kupitia wapatanishi na Iran haikutelekeza diplomasia, lakini “ripoti kuhusu Iran kuomba majadiliano na Amerika ni za uongo,” alisema Baghaei.

“Hii haimo katika DNA yetu.”

Tehran vilevile iliashiria ingali inadhibiti mkondo muhimu zaidi wa maji na masoko ya nishati duniani.