Siasa

Wapiga kelele wa kulipwa waongezeka eneo la Luo Nyanza

Na GEORGE ODIWUOR April 7th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MWENENDO ambapo wanasiasa sasa wanazomewa katika majukwaa ya mikutano unaendelea kushuhudiwa huku kampeni za uchaguzi wa 2027 zikishika kasi.

Baadhi ya wanasiasa ambao wamekuwa wakipinga Serikali Jumuishi kutoka eneo la Luo Nyanza, kwa mfano, wamekuwa wakizomewa katika mikutano ya kisiasa.

Kwa upande mwingine, wale ambao ni wa ODM lakini si wachapakazi licha ya kuwa uongozini kwa kipindi kirefu, pia hawajasazwa.

Mnamo Machi 24, Gavana wa Siaya, James Orengo alizomewa wakati wa ziara ya maendeleo ya Rais William Ruto katika gatuzi hilo.

Bw Orengo alijipata akiimbiwa wimbo wa ‘Tutam’ katika mkutano uliofanyika katika ufuo wa Usenge.

Gavana huyo amekuwa mwiba kwa wanasiasa wa ODM ambao wanaunga mkono Serikali Jumuishi huku akiegemea mrengo wa Linda Mwananchi.

Baada ya kuona amelemewa na wananchi, Bw Orengo alinywea na kusema anamkaribisha Rais Ruto arudi Siaya kwa mara nyingine.

Mwakilishi wa Kike wa Siaya Dkt Christine Ombaka naye alilazimika kukatiza hotuba yake katika uwanja wa Aindi mjini Siaya baada ya kuzomewa kwenye mkutano wa ODM mnamo Februari 21.

Dkt Ombaka amehudumu kama mwakilishi wa kike wa Siaya kwa mihula mitatu kupitia ODM.

Alizomewa kwenye mkutano wa Linda Ground uliokuwa umeongozwa na Kiongozi wa chama hicho, Dkt Oburu Oginga na Gavana wa Homa Bay, Gladys Wanga.

Bi Ombaka alialikwa ahutubu na mbunge wa Bondo Gideon Ochanda.

Ilimlazimu Mbunge wa Alego Usonga Samuel Atandi na Kiongozi wa Wachache Bungeni Junet Mohamed kuingilia kati ili kuwatuliza raia na kumruhusu Dkt Ombaka ahutubu,

Katika Kaunti ya Homa Bay, wafuasi wa wanasiasa wamekuwa wakizomeana, wengine wakibebea vuvuzela na vipenga kwa ajili ya shughuli hiyo katika mikutano ya umma au hafla za mazishi.

Tabia hiyo sasa imeenea zaidi kiasi kuwa wanasiasa wanakodisha mabasi ya kuwasafirisha wafuasi wao ili wahudhurie mikutano na kuzomea wapinzani wao.

Mwakilishi wa Kike wa Homa Bay Joyce Osogo Bensuda ameshutumu tabia hii akisema wanasiasa na wafuasi wao wanastahili kufahamu kuwa Kenya ni taifa ambalo msingi wake ni demokrasia na kuvumilia maoni kinzani.

“Tuko katika nchi ya kidemokrasia na haimaanishi kuwa ukitaka kushindana nami lazima uwalipe wanawake waje wanipigie kelele,” akasema Bi Osogo.

Mbunge huyo maarufu kwa wakazi wa kaunti hiyo kama ‘Opug Nyasungu’ alisema wanaotumia siasa za kuzomeana hawana hekima akisema mtindo huo hauwezi kumsaidia mwanasiasa kupata nafasi ya uongozi.

“Kuzomeana kunaonyesha tu huna hekima na unapoteza wakazi wako bure. Tushindane kwa sera badala ya vitisho na kelele ambazo zinaongeza tu uhasama,” akaongeza.