Patachimbika hapa mbele? ODM, UDA katika vita vikali kuhusu kutengeana ngome
VYAMA vya ODM na UDA sasa vipo kwenye mzozo mkali kuhusu msimamo wa chama hicho cha chungwa kuwa chama tawala kisiwe na wagombeaji katika ngome zake.
Viongozi wa ODM sasa wanamtaka Rais William Ruto na Seneta wa Siaya Dkt Oburu Oginga kuzungumzia suala hilo ili lisizue mgawanyiko zaidi.
ODM inataka wawaniaji wake pekee waruhusiwe kugombea katika ngome zake huku ikiwaachia wale wa UDA eneo la Bonde la Ufa.
Wanasiasa wa UDA hasa kutoka Luo Nyanza wanasema kuwa matakwa ya ODM yatawazuia wananchi kuwachagua viongozi wanaowataka.
Katibu Mkuu wa UDA Hassan Omar amepinga pendekezo hilo akisema nguvu za kila chama lazima zipimwe kwenye debe.
“ODM inadai wao ni chama chenye nguvu zaidi na wanataka watengewe maeneo. Tukutane debeni,” akasema Bw Omar.
Wikendi iliyopita mbunge wa Alego Usonga Samuel Atandi, Eve Obara (Kabondo Kasipul) na mwenzake wa Homa Bay mjini Peter Kaluma waliapa kuwa ODM pekee ndicho chama kitakachokuwa na wagombeaji Nyanza na ngome zake nyingine za kisiasa.
“Hapa hakuna mjadala. Makubaliano yetu na UDA lazima yashirikishe sisi kuachiwa ngome zetu,” akasema Bw Atandi wakati wa ibada ya kanisa kwenye eneobunge la Muhoroni wikendi.
Mbunge Mwakilishi wa Kike wa Kisumu Ruth Odinga naye alisema ODM inastahili kulinda ngome za kisiasa na wakati huo huo pia iwe na wagombeaji kwenye nyadhifa zote.
Ngome
Bw Kaluma alisisitiza kuwa ngome za kisiasa za ODM hazifai kuingiliwa akitoa mfano wa Kaunti ya Homa Bay.
“Sisi malengo yetu hapa Homa Bay ni kuwa washikilizi wote wa viti watoke ODM,” akasema Bw Kaluma.
Hata hivyo, wagombeaji wa UDA nao wameapa kwamba hawatatetereka na watakuwa debeni dhidi ya wenzao wa ODM.
Katika eneobunge la Kasipul, wawaniaji Festus Juma, Fredrick Abala ambaye ni katibu mtendaji wa UDA na mgombeaji wa kiti cha udiwani wa Kasipul Magharibi Ken Chiaga wote wamepinga pendekezo la ODM kuachiwa viti katika Kaunti ya Homa Bay.
Bw Juma alidai kuwa ODM huenda inakisia kuwa itapoteza viti vingi kutokana na kutokwepo kwa marehemu Kinara wao Raila Odinga ndiyo maana inasisitiza iachiwe viti.
“Homa Bay si ngome ya ODM tena na lazima wanasiasa wote waruhusiwe washindane kwa haki na uwazi. Tunataka vyama vyote viwe na wawaniaji ili wananchi wamchague kiongozi wanayemtaka,” akasema Bw Juma.
Bw Bala naye alisema Katiba ya Kenya inaruhusu kila mtu kuwania nafasi ya uongozi kwa njia huru huku akiwataka wapigakura wasizingatie shinikizo kutoka kwa wanasiasa.
“Wamekuwa wakitegemea mbinu za wawaniaji wote sita kupigiwa kura kwa tiketi ya chama kimoja. Mara hii mambo yatakuwa tofauti na nina imani kwamba UDA itajizolea viti vingi hapa Homa Bay,” akasema Bw Bala.
Bw Chiaga alisema kwamba kuwa na wawakilishi kutoka chama kimoja ndiko kumekuwa kukiwazuia wawakilishi wadi wa Homa Bay kutathmini utendakazi wa kina wa Gavana Gladys Wanga.