Trump ageuka debe tupu, akubali mazungumzo na Iran
WASHINGTON, AMERIKA
PAKISTAN Jumatano asubuhi ilifaulu kushawishi Amerika na Iran zisitishe vita kwa muda wa wiki mbili kupisha mazungumzo.
Rais wa Amerika Donald Trump alitangaza kuwa nchi hizo hazitashiriki vita kwa muda huo.
Alitoa tangazo hilo saa chache kabla ya kutekeleza vitisho vyake vya kuishambulia Iran iwapo nchi hiyo ingekataa kufungua Strait of Hormuz.
Trump alisema msingi wa mkataba huo ulikuwa ni Iran kuruhusu meli zipite Strait of Hormuz ambako humusi ya mafuta ya ulimwengu hupitia.
Njia ya Strait of Hormuz haijakuwa ikipitika tangu Amerika-Israel zilivamie Iran Februari 28.
Baraza la Kuu la Kitaifa la Usalama na Dini Iran zilisawiri makubaliano kama ushindi dhidi ya Amerika-Israel. Baraza hilo lilisema Amerika ilikuwa imekubali masharti yake kabla ya kusitisha vita.
Waziri Mkuu wa Pakistan Shehbaz Shariff alichapisha kwenye ukurasa wake wa X kuwa alikuwa amealika wajumbe wa Iran na Amerika kwa mkutano mnamo Ijumaa jijini Islamabad.
Stephane Dujarric, Msemaji wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Kitaifa (UN) Antonio Guterres alitoa wito kwa pande zote kutumia wiki hizo mbili kuelewana na kumaliza vita kabisa Mashariki ya Kati.
“Pande zote ziheshimu yaliyomo kwenye makubaliano ya kusitisha vita kwa sababu amani inahitajika ili kuyalinda maisha ya binadamu na kuyazuia mateso zaidi,” akasema Guterres.
Waziri Mkuu wa Uingereza Keir Starmer alisema ulimwengu angalau utapumua kwa wiki mbili baada ya vita vikali Mashariki ya Kati tangu Februari 28.
“Sote tushirikiane kuhakikisha amani ya kudumu inapatikana kwa sababu kuendelea kwa vita hivi ni hasara sana kwa ulimwengu. Amani ikiwa hata Strait of Hormuz itafunguliwa,” akasema Starmer.
“Hii inastahili kuwa hatua ya kwanza ya kupatikana kwa amani ya kudumu kuepuka zaidi athari ya vita hivyo,” akasema Waziri wa Masuala ya Nje wa Ujerumani Johann Wadephul.
Mkuu wa Sera katika Umoja wa Ulaya (EU) Kaja Kallas alisema kuwa hawatarajii makombora na vitisho ndani ya kipindi hicho.
“Strait of Hormuz itafunguliwa tena na meli zisafirishe mafuta kama zamani na amani ya kudumu ndiyo itahakikisha ulimwengu unasalia dhabiti,” akasema Kallas.
Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu aliunga mkono kusitishwa kwa vita lakini ikasema itaendelea kushambulia Lebanon.
Netanyahu alisema wanaunga mkono Amerika na kutaka Iran ifungulie Strait of Hormuz, ikome kurusha makombora Israel na kambi za kijeshi za Amerika katika mataifa mbalimbali ukanda wa Mashariki ya Kati.
Israel imekuwa ikishambulia Lebanon ambapo zaidi ya watu 1,500 wameuawa na wengine milioni 1.2 kujeruhiwa.
Lebanon iliingizwa kwenye mzozo huo baada ya Hezbollah kurusha roketi Israel kama njia ya kudhihirisha wanaunga mkono Iran siku mbili baada ya kuanza kwa vita.