Fataki tupu Gachagua akimkaba Ruto mbele ya umma mazishi ya Kiaraho
RAIS William Ruto na aliyekuwa Naibu wa Rais Rigathi Gachagua jana walijibizana vikali katika Kaunti ya Nyandarua, tukio ambalo lilionyesha uhasama wa ndani zaidi wa kisiasa unaoendelea kutokota kati yao kuelekea uchaguzi mkuu ujao.
Wawili hao jana walihudhuria hafla ya mazishi ya Mbunge wa Ol Kalou, David Njuguna Kiaraho katika uwanja wa Ol Kalou.
Hii ilikuwa mara ya kwanza ambapo viongozi hao walikutana katika hafla ya wazi tangu mwaka wa 2024.
Bw Gachagua katika hotuba yake alimlenga Rais Ruto moja kwa moja akisema kuwa hata kama alihusika katika kumbandua madarakani, hawezi kumaliza ufuasi wake katika ukanda wa Mlima Kenya.
“Ulifaulu kuniondoa afisini lakini jinsi unavyoona watu wa Mlima Kenya bado wananipenda na bado niko kwenye roho zao,” akasema Bw Gachagua baada ya kualikwa kuhutubu.
“Wakati nilikuwa nikitolewa afisini marehemu Kiaraho alitishwa na akatakiwa kushiriki mchakato wa kuniondoa ila alisimama kidete. Wabunge wengine walilipwa wanisaliti lakini hakunisaliti, ndiyo maana niko hapa kumwomboleza,” akaongeza Bw Gachagua.
Aidha, kiongozi huyo wa chama cha DCP alimtaka Rais Ruto aingilie kati na kuwadhibiti wanasiasa wandani wake kutoka Mlima Kenya, akimtaja Kiongozi wa Wengi Kimani Ichung’wah.
“Sote tulikupigia kura lakini kuelekea 2027 itabidi ututhibitishie kuwa unahitaji kura zetu. Uliwasaliti watu wetu na ukapoteza heshima waliyokuwa wamekupa,” akaongeza.
Rais Ruto aliposimama kuzungumza huku akitetea rekodi ya maendeleo ya serikali yake, alimshutumu Bw Gachagua kwa kushiriki siasa za mgawanyiko na za kikabila.
“Ikifika 2027 viongozi wote watatathminiwa kutokana na utendakazi wao. Nawaomba viongozi wote wakome kuendeleza maslahi yao ya kibinafsi na kuzua mgawanyiko kati yangu na watu walionipigia kura. Watu wa Mlima Kenya ni werevu sana,” akasema Rais Ruto.
Seneta wa Nyandarua, John Methu ndiye aliyekuwa wa kwanza kuzungumza ambapo aliwashutumu wandani wa Rais Ruto kwa kumtusi Bw Gachagua kila mara kwenye hafla za umma.
“Nakuheshimu Rais lakini sikuogopi,” akasema Bw Methu, kauli iliyochangamsha waombolezaji waliomshangilia.
Bw Methu ambaye alimrejelea Bw Gachagua kama naibu rais wa wananchi, aliwataka viongozi ambao wamekuwa wakimtusi Bw Gachagua wafanye hivyo wakati wa ibada hiyo.
“Kimani Ichung’wah jaribu kumtishia au kumtusi Bw Gachagua hapa. Hapa Nyandarua utaona moto sana, jaribu,” akasema seneta huyo akishangiliwa.
Seneta huyo alipanda jukwaani baada ya kukaribishwa na Mwenyekiti wa Kamati ya mazishi ya Bw Kiaraho, Kwenya Thuku ambaye pia ni mbunge wa Kinangop.
“Hivi ndivyo ulimpenda Rigathi Gachagua? Kiongozi ambaye anachukiwa, anatusiwa na alifurushwa?” akauliza huku akiendelea kuwaandama Rais Ruto na wandani wake.
Akionekana kupandwa na mori, seneta huyo aliishutumu serikali kwa kutelekeza miradi ya maendeleo katika Kaunti ya Nyandarua akihusisha hilo na siasa.
“Uliahidi kuwa utawala wako utaimarisha barabara mbalimbali hapa. Umefanya hivyo?” akauliza Bw Methu.
Pia aliwashukuru waombolezaji kwa kukataa kumwaibisha Bw Gachagua kwenye mazishi hayo.
“Tunasikia kuna watu waliletwa kutuzomea lakini mmetuonyesha mapenzi na kudhihirishia ulimwengu mzima jinsi ambavyo mnampenda Gachagua na wanasiasa wanaomuunga mkono,” akasema.
Familia ya Bw Kiaraho ilimsifu baba yao kama kiongozi ambaye alimakinika sana kutekeleza huduma kwa watu waliomchagua na wakaashiria kuwa mwanawe marehemu atajiunga na siasa hivi karibuni.
“Tumekujua tangu 2013 na baba alituambia wewe ni mtu mwaminifu sana. Ulisimama naye tangu 2013 hadi alipoaga dunia na nakuhakikishia Rais familia yetu iko nyuma yako,” akasema Kiaraho.
Mkewe Kiaraho, Jackline alimsifu mumewe kutokana na uongozi wake na akasema mwanawe yuko tayari kuchukua usukani kutoka kwa babake ambaye alimfunza siasa kwa zaidi ya miaka 10.