Siasa

Sifuna arejea kwa jopo la mizozo ya vyama kuzuia jaribio jipya la kumtimua ODM

Na JOSEPH WANGUI, DANIEL OGETTA April 9th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

SENETA wa Nairobi, Edwin Sifuna amerejea katika Jopo la Kutatua Mizozo ya Kisiasa (PPDT) akiomba alindwe dhidi ya juhudi mpya za kumtimua kama Katibu Mkuu wa ODM.

Kwenye ombi lake, Bw Sifuna anataka jopo hilo lisitishe utekelezaji wa uamuzi wa chama wa Februari 11 ambao ulimbandua madarakani.

Pia anataka mchakato wa kusikilizwa kwa kesi ya nidhamu dhidi yake kwa kufika mbele ya jopo la nidhamu, usitishwe.

Alisema chama kimekumbatia mchakato ambao matokeo yake yashafahamika licha ya maagizo ya hapo awali ya PPDT kuwa ODM isuluhishe mzozo huo naye kupitia mifumo ya ndani ya chama.

Bw Sifuna alienda kwenye jopo hilo baada ya Mwenyekiti wa ODM, Gladys Wanga kumwandikia barua wiki iliyopita akimtaka ajibu madai ya ukosefu wa maadili dhidi yake na pia afike mbele ya jopo la nidhamu.

Anadai uamuzi wa Baraza Kuu la Chama ambao ulimwondoa madarakani ulikiuka haki yake ya kusikilizwa.

“Uamuzi huo uliafikiwa bila mimi kufahamishwa kuhusu madai yoyote na pia sikupewa nafasi yoyote ya kujitetea,” akasema Bw Sifuna kwenye barua yake.

Tofauti kati ya Bw Sifuna na ODM zilitokana na hatua ya chama kumwondoa kwenye wadhifa wake baada ya mkutano wa Baraza la Kitaifa la chama mnamo Februari 11.

Bw Sifuna anasema suala hilo hata halikuorodheshwa kwenye ajenda ya mkutano wala hakufahamishwa kabla ya uamuzi huo kufanywa.

Alipoelekea kwa PPDT, ODM iliamrishwa itatue suala hilo kwa kufuata sheria za chama ndipo Bi Wanga akamwandikia Bw Sifuna barua za kumtaka ajitetee.

Bw Sifuna sasa anadai mchakato mbele ya kamati ya nidhamu ushaingiliwa na matokeo yake yashajulikana, akisema chama kinalenga tu kumtimua.

Alishangaa kwa nini aliandikiwa barua ya kujibu na wakati huo huo chama kilishatenga tarehe ya kusikilizwa kwa hatua za kinidhamu dhidi yake.

Pia ameshambulia ODM kwa kuchukua miezi miwili kabla ya kuorodhesha malalamishi dhidi yake na kukosa kuwasilisha stakabadhi za mashtaka dhidi yake.

Katika kesi hii sasa anataka PPDT isitishe mchakato wote wa nidhamu dhidi yake na pia uamuzi ulioafikiwa na NEC wa kumbandua madarakani uharamishwe.

Hatua ya Bw Sifuna kurejea PPDT sasa inaliacha jopo hilo na kazi ngumu ya kuamua mzozo huo badala ya kuuachia chama.

Kesi aliyowasilishwa iliorodheshwa kama ya dharura na itasikizwa leo saa nane unusu mchana.