Habari

Kenya yageuka ‘paradiso’ ya vurugu na uhuni

Na JUSTUS OCHIENG April 11th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

INGAWA watu watatu wanaodaiwa kuhusika na shambulio dhidi ya Seneta wa Vihiga, Godfrey Osotsi, mjini Kisumu, walifikishwa kortini, ukweli unabaki gizani, kwamba wahuni wanaohusishwa na wimbi linaloongezeka la vurugu zilizopangwa nchini Kenya bado hawajulikani.

Kila uvamizi wa mali, kila shambulio katika ibada makanisani na kila tukio la kushambuliwa kwa watu binafsi, kuna wafadhili, wasimamizi na watekelezaji wa moja kwa moja.

Mtandao huu unalindwa na siasa, mamlaka na ukosefu wa uwajibikaji, na umejikita katika kile kinachotajwa kama “uchumi wa vurugu.”

Swali kuu ni nani anaamuru shambulio kama hayo yatekelezwe.
Seneta Osotsi alishambuliwa mchana peupe katika kituo cha biashara mjini Kisumu, tukio lililorekodiwa na kamera za CCTV na kushuhudiwa na watu wengi.

Kulingana na wachunguzi na mashahidi, tukio hilo halikuwa la ghafla bali lilipangwa kwa umakini na kutekelezwa kwa njia ya kitaalamu, likionyesha uwepo wa mfumo uliokomaa wa utekelezaji wa vurugu.

Ndani ya saa chache baada ya tukio hilo, maafisa wa Idara ya Upelelezi wa Jinai (DCI) waliwakamata washukiwa watatu, akiwemo Carlos Owiti, Eric Otieno na Vincent Odhiambo.

Hata hivyo, hatua hiyo imeonekana kugusa tu sehemu ndogo ya mtandao mkubwa wa vijana wanaoajiriwa kwa malipo kuzua vurugu kwa niaba ya watu wenye ushawishi.

Tukio hilo linaungana na matukio mengine ya kihistoria ya kisiasa nchini Kenya.

Mwaka wa 2023, shamba la Northlands linalomilikiwa na Rais mstaafu Uhuru Kenyatta lilivamiwa na mali kuharibiwa.

Baadaye, kampuni ya Spectre inayohusishwa na familia ya Raila Odinga ililengwa.

Mwaka 2021, msafara wa Rais William Ruto, akiwa Naibu Rais wakati huo, ulipigwa mawe Kisumu.

Mwaka 2026 pia kumekuwa na matukio ya vurugu dhidi ya viongozi katika maeneo ya Kisumu na viunga vyake, hali inayoashiria kuongezeka kwa siasa za makundi na uhasama uliopangwa.

Mwezi uliopita, mali inayohusishwa na Raphael Tuju na Irungu Nyakera ilivamiwa na makundi ya wahuni, huku makanisa katikamaeneo ya Mwiki, Kariobangi na Othaya yakivurugwa na watu wenye silaha.

Wachambuzi wa haki za binadamu wanasema majibu ya serikali yamekuwa ya kauli kali lakini utekelezaji wake dhaifu.

Wanaeleza kuwa tatizo hili limechochewa na siasa za upendeleo, ukosefu wa uwajibikaji na ulinzi wa kisiasa kwa wahusika wakuu.

Kwa mujibu wa Kituo cha Utafiti wa Uhalifu (NCRC), Kenya ina takriban magenge 309 ya uhalifu yaliyoenea katika kaunti mbalimbali, huku Nairobi, Mombasa na Kisumu zikiwa na idadi kubwa.

Magenge haya yameacha kuwa ya muda na sasa yamegeuka taasisi za kudumu ndani ya jamii.

Katika enzi ya sasa, “uchumi wa wahuni” umepata sura mpya ya kidijitali.

Baadhi ya wahuni sasa hujipatia umaarufu mitandaoni kupitia TikTok, X na Facebook, wakionyesha vitendo vyao au vitisho .

 

wanavyotekeleza. Hali hii imewageuza kuwa bidhaa katika soko la siasa na propaganda.

Wataalamu wanaonya kuwa tatizo hili linachochewa na ukosefu wa ajira kwa vijana, tofauti kubwa ya kiuchumi na ufisadi uliokita mizizi.

Wanasema kukamata wahusika wa chini pekee haitoshi bila kuwawajibisha wafadhili na waagizaji wa vurugu hizo.

Kenya inapoelekea katika uchaguzi mkuu ujao, hofu inaongezeka kuwa mtandao huu wa vurugu unaweza kuimarika zaidi na kuendelea kuathiri demokrasia, biashara na utawala wa sheria nchini.