Habari za Kitaifa

SAKATA YA MAFUTA: Wandayi kujibu maswali magumu 16 bungeni Jumanne

Na SAMWEL OWINO April 12th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

ANGALAU maswali 16 yanamsubiri Waziri wa Kawi, Opiyo Wandayi, bungeni Jumanne kuhusu uingizaji wa shehena ya tani 60,000 za petroli iliyoingizwa nchini nje ya mfumo wa Serikali kwa Serikali (G-to-G).
Baada ya kushindwa kufika mbele ya wabunge Alhamisi, Wandayi ameitwa na Kamati ya Bunge ya Kawi kueleza kuhusu sakata hiyo ya mafuta na uhaba wa bidhaa hiyo unaokumba sehemu mbalimbali za nchi.
Sakata hiyo tayari limesababisha kujiuzulu kwa maafisa wakuu wa sekta ya kawi akiwemo aliyekuwa Katibu wa Nishati Mohamed Liban, aliyekuwa Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Kuthibiti Kawi na Petroli (EPRA) Daniel Kiptoo, na aliyekuwa Mkurugenzi Mkuu wa Kenya Pipeline Company Joe Sang.
Barua ya kamati inayoongozwa na Mbunge wa Nakuru Mashariki David Gikaria inaeleza kuwa Wandayi anatakiwa kutoa maelezo ya kina kuhusu idhini maalum zilizotolewa kuruhusu uingizaji wa mafuta hayo na ni nani aliyeruhusu kuingia kwake nje ya mfumo wa G-to-G.
Kamati pia inataka kuthibitisha stakabadhi za idhini, mawasiliano ya wizara na EPRA, na iwapo kulikuwa na idhini ya maandishi au ya mdomo.
Waziri huyo, pamoja na Mkurugenzi Mkuu mpya wa EPRA Joseph Oketch, maafisa wa Kenya Pipeline Company na Mamlaka ya Ukusanyaji Ushuru Kenya (KRA), wanatakiwa kueleza ni wapi hasa mchakato wa ukaguzi wa ubora wa mafuta ulifeli.
Wabunge wanataka kujua kama ukaguzi wa kabla ya usafirishaji ulifanyika, ni nani aliyehusika, matokeo yake yalikuwa gani, na ni nani alitia saini vyeti vya mwisho vya ubora.
Pia wanataka kujua kama hatua zozote zimechukuliwa dhidi ya waliohusika.
Kamati imehoji pia iwapo mafuta hayo yaliingia kwenye mfumo wa usambazaji kupitia bandari na mabomba bila uthibitisho huru, na ni wapi hasa katika mfumo wa usambazaji taratibu zilivunjwa.
Wabunge wanataka kujua ni viwango gani vya ubora vilikiukwa na kwa nini mapungufu hayo hayakugunduliwa kwa wakati.
Aidha, Wizara ya Nishati na EPRA zinatakiwa kueleza iwapo mifumo ya ufuatiliaji wa mafuta ilikiukwa au ilidukuliwa, na ni maafisa gani wamebainika kuwa na hatia hadi sasa.
Kamati pia inataka kujua ni hatua gani za kinidhamu au kisheria zimechukuliwa, na lini matokeo ya uchunguzi yatatangazwa kwa umma.
Wabunge wamesema ni lazima pia ijulikane iwapo mafuta yasiyokidhi viwango yaliingia sokoni na ni kiasi gani tayari kimefikia wananchi.
“Ni lazima tujue ni nini kilikosekana katika mfumo huu,” imeeleza barua hiyo.
Mbunge wa Bomachoge Borabu Obadiah Barongo amesema kutofika kwa Waziri ni dalili ya kushindwa kuwajibika wakati taifa linakabiliwa na changamoto kubwa ya mafuta.