Ongezeko la magenge ya kisiasa latishia uchaguzi 2027
MWAKA mmoja kabla ya Wakenya kuelekea kwenye debe kuwachagua viongozi wao, ongezeko la magenge yanayotumiwa katika siasa limeibua hofu kuwa makundi hayo yanaweza kuhatarisha uchaguzi mkuu wa 2027.
Wataalamu wa masuala ya usalama, watafiti na wadadisi wa masuala ya kisiasa wanaonya kuwa vijana wasio na ajira wanazidi kutumiwa kuvuruga mikutano ya kisiasa, kuwatisha wapinzani na kuchochea vurugu.
Usajili mara nyingi huanza kwa simu au ujumbe wa WhatsApp unaowaelekeza vijana mahali pa kukutana.
Kwa muda mfupi, mamia ya vijana wanaweza kukusanywa kutoka mitaa na mitaa duni, baadhi wakiahidiwa malipo madogo huku wengine wakifahamu kazi yao baada ya kufika.
Utafiti wa Taifa Leo unaonyesha kijana anaweza kulipwa Sh500 kuhudhuria mkutano, kushangilia au kuongeza idadi ya umati.
Kazi hatari zaidi, kama kuvuruga mikutano na kukabiliana na makundi pinzani, hulipwa kati ya Sh2,000 na Sh5,000.
Ripoti ya Wakfu wa Kofi Annan iliyotolewa Julai ilikadiria uwezekano wa kutokea kwa ghasia zinazohusiana na uchaguzi wa 2027 kuwa asilimia 84.1.
Ripoti hiyo ilitaja ukosefu wa ajira kwa vijana, matatizo ya kiuchumi, ukabila, malalamishi ya kisiasa na kutoaminika kwa taasisi za serikali kuwa baadhi ya sababu zinazoweza kuchochea vurugu.
Ripoti ya OdipoDev na Tribeless Youth ya 2025, Goonland: Looking Beyond the Money and Violence in the Political Exploitation of Young Men, ilieleza magenge hayo kama soko lisilo rasmi ambako vurugu hununuliwa na kuuzwa.
Peter Ouko, mkurugenzi wa shirika la Crime Si Poa (Uhalifu si mzuri), alisema tatizo si vijana wanaotumiwa pekee, bali pia wafadhili wao.
“Wanasiasa ndio wanapaswa kulaumiwa kwa kudumisha tabia hizi. Kila mhuni ana mtu anayemkodi,” akasema Ouko.
Kituo cha Kitaifa cha Utafiti wa Uhalifu (NCRC) kiliripoti mnamo 2025 kuwa kulikuwa na magenge 73 Mombasa, 56 Nairobi na 47 Kilifi.
Baadhi yanadaiwa kuungwa mkono na wanasiasa na kutumika kama walinzi wa kisiasa.
Mkurugenzi wa NCRC Dkt Mutuma Ruteere asema ni muhimu kuwachunguza wanaoendesha magenge hayo badala ya kuwafuatilia majambazi pekee.
Tume ya Kitaifa ya Uwiano na Utangamano (NCIC) nayo imeonya kuwa magenge yanazidi kuwa na uhusiano na siasa.
Hofu hiyo iliongezeka baada ya vurugu za uchaguzi mdogo wa Ol Kalou Julai, ambapo makundi yenye silaha yaliwashambulia wakazi, wanahabari na wafuasi wa kisiasa, huku watu wawili wakiuawa.
Waziri wa Usalama wa Ndani Kipchumba Murkomen alikiri kuwepo kwa magenge ya kisiasa, lakini akasema hali si mbaya kama ilivyoelezwa.
Katibu katika wizara hiyo, Dkt Raymond Omollo, alisema ukosefu wa ajira kwa vijana umechangia tatizo hilo na serikali inaongeza fursa kupitia mipango kama NYOTA.
Hata hivyo, wachunguzi wanaonya kuwa iwapo mitandao hiyo haitadhibitiwa kabla ya kampeni kushika kasi, tishio kubwa halitakuwa vurugu pekee, bali pia doa katika uchaguzi mkuu wa 2027.