Makala

Papa wa Roma anavyomudu mawimbi ya siasa Kenya

Na BENSON MATHEKA April 12th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

SIASA za kuelekea uchaguzi mkuu wa 2027 zinapoanza kupamba moto katika kanda ya Bonde la Ufa na Magharibi mwa Kenya, jina la Moses Masika Wetang’ula limeibua mjadala sio tu maeneo hayo bali pia kitaifa.

Wetangula, anayejulikana kwa jina la utani Papa wa Roma, ana wasifa wa kuwa wakili, waziri na sasa Spika wa Bunge la Kitaifa.

Hata hivyo, katika mazingira ya Serikali Jumuishi anakabiliwa na changamoto ya kuoanisha wajibu wake wa kikatiba na malengo binafsi ya kisiasa.

Tangu ateuliwe spika Wetang’ula amejijengea taswira ya kiongozi anayehudumia umma, safari iliyoianza zaidi ya miaka 40 iliyopita.

Kuanzia uteuzi wake kama hakimu mwaka 1982 hadi kuwa mbunge kwa zaidi ya miaka 30 katika eneobunge la Sirisia na seneta wa kwanza wa Bungoma, ameonyesha ustahimilivu wa kisiasa usio wa kawaida.

Kwa mujibu wa mchanganuzi wa masuala ya kisiasa Victor Muniafu, Spika Wetang’ula ni mtaalamu wa taratibu za Bunge.

“Ni mtu ambaye amesakata mchezo huu kwa muda mrefu. Hajibu tu presha za kisiasa bali huziyeyusha na kuzitumia kujijenga zaidi,” anahoji.

Muafaka wa kisiasa kati ya William Ruto na Raila Odinga uliozaa Serikali Jumuishi umebadili pakubwa mwelekeo wa siasa za Bunge.

Ingawa umeondoa migongano kati ya vyama hivyo viwili, pia umeweka mzigo mkubwa kwa Spika kuhakikisha ushirikiano huo unadumu ikizingatiwa kwamba yeye ni mmoja wa vinara wa muungano tawala wa Kenya Kwanza.

Kwa mujibu wa mshauri wa masuala ya utawala Sheila Mwangi, kwa kiwango kikubwa Wetang’ula ndiye kiungo muhimu kinachoshikilia handisheki hiyo.

“Muungano wa UDA na ODM ni wa maslahi, lakini jukumu la Spika ni kuhakikisha unafanya kazi. Yeye ndiye nguzo ya uthabiti katika hali ambayo inabadilika kila mara,” anasema.

Hata hivyo, wakosoaji wanahoji kwamba wadhifa wake kama Spika pamoja na yeye kuendelea kuwa kinara wa chama cha Ford Kenya unaweza kuathiri jukumu lake la kutopendelea upande wowote.

Licha ya changamoto hizo Wetang’ula amesisitiza kuwa anazingatia haki na usawa katika uongozi wake, akirejelea katiba ambayo haimzuii kushikilia nyadhifa zote mbili.Kinachozua mjadala zaidi ni dalili za azma yake ya kisiasa baada ya 2032.

Kauli kutoka kwa washirika wa karibu wa Rais Ruto zimeashiria uwezekano wa Wetang’ula kuwa miongoni mwa watu wanaoweza kumrithi rais siku zijazo.

Mchanganuzi wa siasa Nathan Kagwanja anaamini kuwa hatua za Wetang’ula si za bahati nasibu: “Haangalii 2027 pekee bali pia 2032. Kwa kudumisha chama chake na nguvu zake bungeni, anajisawiri kama mpangaji mkuu wa siasa za baadaye, au hata kiongozi mwenyewe wa siasa hizo.”

Kwa sasa Wetang’ula anaendelea kuzunguka maeneo mbalimbali ya nchi akijenga ushawishi wake ili uvuke mipaka ya ngome yake ya Bungoma.

Iwapo atabaki mwamuzi huru bungeni au atajitosa wazi wazi katika mbio za kunasa kiti cha juu kabisa cha kisiasa – urais – bado ni swali linalosubiri majibu.

Lakini jambo moja ni wazi; katika siasa za sasa Moses Masika Wetang’ula si mtu wa kupuuzwa.