Dimba

Nyota Victor Wanyama aomba sapoti kwa mkewe staa mwigizaji Teshna

Na SINDA MATIKO April 12th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

NYOTA wa soka mstaafu Victor Wanyama ameomba mashabiki kusapoti mke wake Serah Teshna kwenye harakati zake za uigizaji.

Juzi kati kwenye uzinduzi wa filamu ya kwanza ya Teshna kama prodyusa, Buss 338, Wanyama alikuwa miongoni mwa wageni walioalikwa kuhudhuria hafla hiyo jijini Nairobi.

“Nimependezwa sana kuona jinsi umati mkubwa ulijitokeza ili kuja kumsapoti (Teshna) kwenye uzinduzi wa filamu hii. Pia mastaa kibao waigizaji wamejitokeza na hilo ni jambo la kutia moyo,” alitanguliza Wanyama.

“Ningependa kuona sapoti zaidi si kwa yeye tu bali pia kwa waigizaji na maprodyusa wengine. Watu wanapojitokeza kwa ukubwa huu kusapoti wasanii wanaishia kupiga jeki sekta nzima,” akarai mashabiki na wadau.

Hafla hiyo ilijiri siku chache baada ya Wanyama kutangaza kuwa amestaafu soka ya kulipwa baada ya miaka 19.

Hadi anatoa tangazo hilo nahodha huyo wa zamani wa timu ya taifa Harambee Stars alikuwa amesakata boli kwa miaka miwili toka alipoachana na klabu yake ya mwisho FC Montreal kule Canada.