Kimataifa

Waasi wa Houthi sasa wafungia Saudia bahari katika mbinu ya kuunga mkono Iran

Na REUTERS July 22nd, 2026 Kusoma ni dakika: 2

SANAA, Yemen:

WAASI wa Houthi nchini Yemen wamezitaka kampuni za usafirishaji wa mizigo kwa njia ya bahari kutopakia wala kushusha mizigo katika bandari za Saudi Arabia.

Houthi imeonya kuwa meli zitakazokiuka agizo hilo zitashambuliwa mahali popote ndani ya maeneo yanayofikiwa na vikosi vyao.

Onyo hilo lilitolewa kupitia baruapepe iliyoandikwa Julai 20 na kutumwa kwa kampuni kadhaa za usafirishaji mizigo.

Mnamo Jumatatu, Houthi walitangaza kuwa wamezingira bahari isitumiwe na Saudi Arabia.

Hii ni hatua inayoweza kuzidisha vita kati ya Amerika na Iran huku biashara ya ulimwengu ikivurugika na bei ya mafuta kupanda hata zaidi.

“Meli zote zimepigwa marufuku kupakia au kushusha mizigo katika bandari yoyote ya Saudi Arabia,” ikasema barua hiyo ya Houthis.

Waasi hao wamewashauri manohadha wa meli wachukue tahadhari kubwa kabla ya kushiriki shughuli zozote zinazohusisha bandari za Saudi Arabia.

Kwa mujibu wa barua hiyo, masharti hayo mapya yalianza kutekelezwa Julai 20 na kundi hilo limesisitiza litahakikisha yanatiliwa manani.

“Meli zitakazokiuka agizo hili zitakabiliwa na vikwazo. Aidha, zitashambuliwa mahali popote zilipo ndani ya maeneo yanayofikiwa na uwezo wa vikosi vyetu hapa Yemen,” ikasema taarifa hiyo iliyotumwa na Kituo cha Kuratibu Oparesheni za Kibinadamu cha Houthi (HOCC), chenye makao yake jijini Sana’a.

Iwapo njia ya kusini ya Bahari ya Shamu itafungwa, Saudi Arabia itapoteza njia muhimu mbadala ya kufikia Mlango wa Hormuz.

Hali hii inaweza kuongeza hofu ya kupungua kwa mafuta na bidhaa katika soko la dunia.

Usafiri wa meli katika Bahari ya Shamu bado haujarejea kawaida tangu Houthi waanze kushambulia meli za kibiashara mnamo Novemba 2023.

Walitekeleza mashambulizi hayo wakisema walikuwa wanaunga mkono Wapalestina katika vita vya Gaza dhidi ya Israel.

HOCC ndiyo kitengo kilichotumiwa na Houthi kutoa onyo kadhaa kwa sekta ya usafirishaji wa baharini wakati wa mashambulizi dhidi ya meli za kibiashara kati ya 2023 na 2025.

Walikomesha kushambulia meli baada ya makubaliano ya kusitisha mapigano Gaza mnamo Oktoba mwaka jana kufikiwa.

Duru kutoka mojawapo ya kampuni zilizopokea barua hiyo zilisema ujumbe huo unaonyesha kuwa Houthi bado wanataka kudhihirisha kuwa wana uwezo wa kuathiri usafiri wa baharini katika eneo hilo.