Ruto na Gachagua kupimana nguvu tena uchaguzi mdogo
RAIS William Ruto na aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua wanatarajiwa kukabana koo tena kisiasa huku uchaguzi mdogo wa eneobunge la Emurua Dikirr mnamo Mei 14 ukikaribia.
Kinyang’anyiro hicho cha kumrithi marehemu Johana Ngeno, aliyefariki katika ajali ya helikopta pamoja na watu wengine watano katika eneo la Mosop, kaunti ya Nandi, Februari 28, kimevutia wagombea wanne.
Mgombea wa chama cha United Democratic Alliance (UDA), David Kipsang Keter, atamenyana na Vincent Kibet Rotich wa chama cha Democracy for Citizens Party (DCP) kinachoungwa mkono na Bw Gachagua. Wawili hao wanachukuliwa kuwa vinara katika kinyang’anyiro kinachotarajiwa kuwa na ushindani mkali.
Wengine katika mbio hizo ni wakili Gideon Koech anayewania kupitia chama cha National Vision Party (NVP) na mfanyabiashara Desma Cherono wa chama cha Party of National Unity (PNU).
Akiwa ametiwa moyo na ushindi wa hivi karibuni wa mgombea wa DCP Douglas Twala Masikonte katika uchaguzi mdogo wa wadi ya Narok Town mnamo Novemba 2025, Bw Gachagua analenga kuimarisha ushawishi wa chama chake katika eneo la Bonde la Ufa kuelekea uchaguzi mkuu wa 2027. Ushindi huo uliashiria mafanikio yasiyotarajiwa kwa DCP katika eneo lililokuwa ngome ya UDA.
Uchaguzi wa Emurua Dikirr pia unafanyika wakati ambapo kuna mgawanyiko ndani ya UDA kufuatia mchujo uliokuwa na ushindani mkali. Bernard Ngeno, aliyekuwa msaidizi wa marehemu Ngeno, amekataa kukubali matokeo baada ya kushindwa kwa kura chache na Bw Keter. Alidai kuwa mchakato huo ulikuwa na dosari na akaahidi kupanga mikakati mipya kuelekea 2027.
Kukiwa na wapigakura 44,447 waliosajiliwa na 27, 503 waliojitokeza katika mchujo, tofauti ndogo ya kura 355 imefichua mgawanyiko mkubwa katika eneo hilo. Hali hii imelazimisha UDA kuongeza juhudi za kuleta umoja kabla ya uchaguzi huo.
Bw Keter amesema tayari yuko mashinani akirai wapigakura na ana imani kuwa chama chake kitashinda kiti hicho. Amewataka wafuasi kumuunga mkono ili kuenzi marehemu mbunge na kukamilisha miradi ya maendeleo aliyoanzisha Ngeno.
Kwa upande wake, Bw Gachagua alimtambulisha Bw Rotich kama “chaguo la wananchi,” akisema ushindani huo ni kati ya “mradi wa Ruto” na matakwa ya wananchi. Bw Rotich alisema wakazi wamechoshwa na siasa za zamani na wako tayari kwa mabadiliko.
Wagombea wengine pia wameeleza ajenda zao, huku Bw Koech akisisitiza maendeleo ya miundombinu na Bi Cherono akitoa wito kwa wakazi kumchagua mwanamke kwa mara ya kwanza.
Uchaguzi huo pia umeathiriwa na uteuzi wa mjane wa marehemu, Saiyanoi Ngeno, kuwa mjumbe wa bodi ya Mamlaka ya ICT kwa kipindi cha miaka mitatu.
Eneo la Emurua Dikirr bado linakabiliwa na changamoto za miundombinu duni, hasa barabara mbovu zinazoathiri usafirishaji wa mazao kama mahindi, maharagwe, nyanya na vitunguu.
Viongozi wa UDA wamesema wana imani chama kitahifadhi kiti hicho, huku Rais Ruto akiahidi kuwa miradi ya maendeleo iliyoanzishwa na marehemu itakamilishwa.