Ruto kuzindua rasmi safari ya Kenya kuwa kama Singapore: Gumzo la ‘Vision 2060’ ni leo
RAIS William Ruto leo, Jumatano Agosti 12, 2026, anaanzisha mchakato wa mazungumzo ya kitaifa kuhusu mustakabali wa Kenya, huku akiwahusisha wataalamu na wananchi katika kuandaa mpango wa maendeleo wa muda mrefu.
Mchakato huo unaanza wakati ambapo nchi tayari inaanza kuangazia mambo zaidi ya Uchaguzi Mkuu wa 2027 na mjadala kuhusu mwelekeo wa uchumi wa Kenya ukizidi kushika kasi.
Lengo ni kuandaa mpango utakaodumu hata serikali zikibadilika na kuepuka hali ya kila serikali kuja na vipaumbele vyake vipya.
Rais Ruto anataka kuandaa mpango utakaopeleka Kenya zaidi ya Ruwaza ya 2030 na kuiweka katika njia ya kuwa nchi yenye uchumi wa kipato cha juu.
Miongoni mwa wataalamu wanaoshiriki mjadala huo ni Profesa Hiroyuki Hino, mwanauchumi kutoka Japan, ambaye anaamini Kenya inaweza kujifunza kutokana na mafanikio ya kiuchumi ya nchi kama Singapore, Korea Kusini na Vietnam.
Profesa Hino amefanya kazi na Kenya tangu miaka ya 1990 alipokuwa mjumbe mkuu wa Shirika la Fedha Duniani (IMF).
Anasema Kenya haipaswi kuangazia pekee ujenzi wa barabara, reli na miradi mikubwa ya miundombinu. Badala yake, anasema nguvu kubwa ya Kenya iko kwa wananchi wake.
“Hoja yangu kuu ni nguvu ya Wakenya binafsi. Kama ilivyokuwa Mashariki mwa Asia, mafanikio ya kiuchumi yalichangiwa sana na nguvu ya watu,” alisema.
Profesa Hino anasema nchi zilizofanikiwa kiuchumi hazikujenga miundombinu pekee.
Ziliweka pia mifumo inayowasaidia watu kufanya kazi kwa ufanisi na kunufaika kutokana na juhudi zao.
Anasema Ruwaza ya 2030 ilifanikisha baadhi ya mambo, hasa katika miundombinu na ukuaji wa uchumi wa kati ya asilimia tano na sita.
Hata hivyo, anasema matunda ya ukuaji huo hayakuwafikia Wakenya wengi wa kawaida.
“Faida za ukuaji wa uchumi hazikuwafikia watu wa kawaida,” alisema.
Anasema mpango mpya unapaswa kupima mafanikio kwa kuangalia huduma kama maji safi na salama, nishati safi ya kupikia, huduma za afya na mapato ya wananchi.
Profesa Hino anaamini safari hiyo itakuwa ngumu sana, lakini inawezekana.
Anasema Kenya pia inapaswa kufikiria upya namna ya kufadhili maendeleo badala ya kutegemea serikali pekee.
Anashauri kuimarisha biashara ndogo, kuongeza uzalishaji na kutumia mbinu mpya za kupata fedha.
Pia anasisitiza ushiriki wa wananchi.
Anasema mpango huo utadumu zaidi iwapo Wakenya watahusika katika kuandaliwa kwake.
“Watu wote wakihusika katika mchakato, wataumiliki mchakato huo na hatimaye kuumiliki mpango wenyewe,” alisema.
Kwa mtazamo wake, umiliki huo unaweza kusaidia mpango mpya kuendelea hata serikali zikibadilika.
Anasema Wakenya hawapaswi kusubiri serikali pekee kutatua matatizo yao.
Badala yake, wanapaswa kushiriki katika kutoa mawazo na mapendekezo ya jinsi changamoto za nchi zinavyoweza kutatuliwa.