Akili MaliMakala

Umekanishaji unavyobadilisha sura ya kilimo Kenya

Na SAMMY WAWERU April 14th, 2026 Kusoma ni dakika: 3

KWA miaka mingi, wakulima Kenya wamekuwa wakitegemea majembe ya mikono na nguvu zao wenyewe kuendeleza shughuli za kilimo.

Kuanzia kupanda, kupalilia, kunyunyizia mimea dawa hadi kuvuna, uzalishaji chakula umekuwa ukitekelezwa kwa njia ya mikono.

Hata hivyo, upepo mpya unavuma mashambani: umekanishaji unachukua nafasi, ukiahidi kuongeza uzalishaji, kupunguza gharama na kuinua hadhi ya mkulima wa kawaida.

Hapo awali, shughuli nyingi za kilimo zilitekelezwa kwa mikono, hali iliyochukua muda mrefu na wakati mwingine kuhatarisha afya ya wakulima—hasa wakati wa kupulizia mimea dawa dhidi ya magonjwa na wadudu waharibifu.

Leo hii, maendeleo ya teknolojia yanaanza kubadili hali hii, huku sekta ya kilimo inayochangia karibu asilimia 22 ya pato la taifa (GDP) ikionyesha dalili za kuimarika.

Katika maeneo yanayozalisha nafaka kwa wingi kama vile ngano na mahindi, wakulima wanaanza kukumbatia matumizi ya mashine za kisasa. Hizi ni pamoja na matrekta ya kupanda, mashine za kupalilia, vifaa vya kunyunyizia dawa pamoja na mashine za kuvuna.

Katika eneo la Eldoret, Kaunti ya Uasin-Gishu, kwa mfano, baadhi ya wakulima wameanza kutumia droni kunyunyizia mimea dawa—hatua inayopunguza gharama na kuongeza ufanisi.

“Kitambo ingetuchukua siku nyingi kulima shamba na hata kuvuna mazao. Hata hivyo, uwepo wa trekta na mashine kama combine harvester umerahisisha kazi kwa kiwango kikubwa,” anasema Sammy Kipchumba, mkulima wa nafaka kutoka Moiben, Uasin-Gishu.

Uasin-Gishu ni miongoni mwa maeneo yanayoongoza kwa uzalishaji wa mahindi, ngano na maharagwe nchini. Katika kipindi cha chini ya miongo mitatu, eneo hilo limepiga hatua kubwa katika kukumbatia umekanishaji, likiwa na idadi kubwa ya matrekta na mitambo ya kisasa ya kilimo.

Mercy Wanjau, Katibu katika Baraza la Mawaziri akihutubu wakati wa uzinduzi wa kituo cha kuuza matrekta aina ya New Holland nchini kupitia ushirikiano wa kampuni ya Inchcape na New Holland, Februari 2026, Nairobi. Picha|Sammy Waweru

Kwa Kipchumba, kumiliki trekta kumemwezesha kupunguza gharama za uzalishaji na kuokoa muda, huku akiongeza mavuno. Hata hivyo, hali si sawa kwa wakulima wengi wadogo kote nchini.

Takriban asilimia 70 ya wakazi wa mashinani bado wanategemea kilimo cha mikono, hali inayochangiwa kwa kiasi kikubwa na gharama ya juu ya mashine za kilimo.

Kwa mfano, trekta jipya la bei nafuu linaweza kugharimu hadi Sh2 milioni—bei ambayo ni juu ya uwezo wa wakulima wengi wadogo.

Ni kwa sababu hiyo serikali imeanzisha juhudi za kuandaa Sera ya Umekanishaji wa Kilimo ili kuhakikisha wakulima wadogo hawabaki nyuma.

“Sera ya Umekanishaji itawatambua wakulima wa mashamba madogo ambao ndio wengi nchini,” anasema Mercy Wanjau, Katibu katika Baraza la Mawaziri.

Katika mahojiano na Akilimali Dijitali, Wanjau anafafanua kuwa sheria hiyo inalenga kufungua fursa mpya za maendeleo kwa wakulima wadogo kwa kuhamasisha matumizi ya mashine na teknolojia za kisasa.

“Tunatarajia sera hii kupitishwa kuwa sheria hivi karibuni baada ya kuwasilishwa bungeni. Itaelekeza tulikotoka kama taifa na tunakoelekea katika sekta ya kilimo,” anasema.

Kulingana na serikali, soko la vifaa vya kilimo nchini linakadiriwa kuwa na thamani ya Sh155 bilioni. Hata hivyo, pengo kati ya upatikanaji wa mashine na uwezo wa wakulima wadogo kununua linaendelea kuwa changamoto kubwa.

Ili kuziba pengo hilo, serikali inashirikiana na sekta binafsi kuhamasisha umekanishaji. Aidha, umekanishaji unahusisha matumizi ya mashine ili kurahisisha kazi na kuongeza ufanisi katika uzalishaji, hasa kwenye kilimo.

Mercy Wanjau, Katibu katika Baraza la Mawaziri (wa pili kutoka kulia) akizindua rasmi kituo cha kuuza matrekta aina ya New Holland nchini kupitia ushirikiano wa kampuni ya Inchcape na New Holland, Februari 2026, Nairobi. Picha|Sammy Waweru

“Hata kama serikali inaendesha mpango wa mbolea ya ruzuku, kuna haja ya kuanzisha mpango kama huo kwa umekanishaji. Ripoti ya kitaifa ya uzalishaji wa mazao ya mwaka 2025 inaonyesha kuwa licha ya kuzalisha tani milioni 4.03 za mahindi, tunaweza kuongeza uzalishaji huu mara tatu kupitia umekanishaji sahihi,” anaeleza Wanjau.

Anaongeza kuwa kwa wanawake wakulima, umekanishaji unamaanisha ukombozi kutoka kwa kazi ngumu za mikono, huku kwa vijana ukifungua fursa mpya za ajira katika sekta ya teknolojia ya kilimo—ikiwemo uendeshaji, utengenezaji na usambazaji wa mashine.

Katika kuunga mkono juhudi hizi, kampuni ya Inchcape Kenya kwa ushirikiano na New Holland, mnamo Februari 2026, ilizindua kituo cha kuuza matrekta aina ya New Holland nchini, hatua inayolenga kuongeza upatikanaji wa mashine hizo.

“Ni muhimu kuwa na mjadala mpana na wakulima kuhusu uzalishaji wa chakula na jinsi ya kuziba pengo lililopo. Hili linawezekana kupitia upatikanaji wa matrekta ya bei nafuu na yanayomfikia mkulima kwa urahisi,” anasema Marion Gathoga-Mwangi, Mkurugenzi Mkuu wa Inchcape Kenya.

Kutokana na gharama ya juu ya matrekta, kampuni hiyo pia inashirikiana na taasisi za kifedha kama NCBA, Equity, Cooperative na Family Bank ili kuwezesha wakulima kupata mikopo kumiliki mashine hizo.

Isitoshe, Inchcape Kenya inapanga kupanua huduma zake kwa kufungua matawi katika maeneo mbalimbali nchini, huku pia ikileta matrekta madogo na mashine zinazofaa wakulima wadogo.

Wadau katika sekta ya kilimo wanaamini kuwa ikiwa umekanishaji utaimarishwa kikamilifu, uzalishaji wa mazao nchini unaweza kuongezeka maradufu—hatua itakayochangia kwa kiasi kikubwa usalama wa chakula na ukuaji wa uchumi.