Jamvi La Siasa

KINAYA: Tupokezwe shahada kwa kuishi Kenya kwa sababu si rahisi!

June 14th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

KENYA ni nchi ya vipindi tu! Mara mshukiwa ananaswa na mamilioni ya fedha zinazoshukiwa kuwa za wizi, unapata ukutani ameandika ‘Mungu ametenda’, yaani amewezeshwa na Mungu. Kwa hivyo sisi tusioweza kuiba tunateswa na shetani?

Mara polisi wanakosa kazi ya kufanya kama vile kuwanasa wahalifu, wanapinduapindua vibanda vya kuchezea kamari na kuviteketeza, tena wanafurahia ndimi za moto zikivuma kama ngoma za kishetani!

Katika visa vyote viwili, maswali yanasalia kichwani mwa Mkenya wa kawaida kama mimi: Hivi polisi wanasema ukweli kuhusu pesa ambazo walipata katika kisa cha mabunda ya noti waliyopata karundikwa chumbani?

Labda walipata rundo zima, wakaficha robo tatu, wakatutangazia robo moja tu, na kwa kuwa tumeishiwa kiasi cha kuona milioni 65 zikiwa nyingi, tunabaki vinywa wazi kwa mshangao?

Tuambizane ukweli, watu ambao wana ujuzi wa kukunja au kukanyaga noti ya Sh50 wanayoangushiwa chini na matatu ikatoweka kabisa, wanaweza kukubali mamilioni yapitie mikononi mwao bila ‘kujisaidia’ na kiasi fulani?

Katika kisa cha vibanda vya kamari kutiwa moto, unataka kuniambia polisi waliacha Sh50, Sh100, Sh200, Sh500 au hata Sh1,000 walizopata humo ziteketee? Kwani wamekinai pesa siku hizi? Wanataka tuwaamini?

Najua dhana ni dhambi, lakini Kenya hii niliyokulia imenifunza mengi, hivyo lazima nikae macho.

Unakumbana na wachuuzi wa viatu usiku, wanakuuzia jozi nzuri tu, ukifika nyumbani unakuta viatu vyote viwili ni vya mguu wa kushoto!

Ukiviangalia vizuri kwa mshangao unagundua kimoja ni cheusi, kingine cha rangi ya kahawia, ila kimepakwa buluu ili kukuhadaa.

Ukivitizama kwa makini tena unagundua kimoja ni kikubwa zaidi, kinaweza kutosha miguu yako miwili, lakini kufikia hapo kimo hakijalishi kwa kuwa tayari umetapeliwa, vyote havivaliki!

Unatanabahi umekwama kwa hakika kwa sababu hata ukirejea ulipovinunua huwezi kumkuta mchuuzi aliyekuuzia, na ukimpata anaweza hata kukupiga.

Kumbuka wachuuzi wana tabia ya waendeshaji bodaboda, wanaweza kukupiga kitutu hata kabla hawajajua kuwa umekosewa, na wakishajua wanakimbia badala ya kukuomba msamaha.

Ukiamua kushtakia hali polisi unakumbuka utaambiwa uweke gari – la serikali – mafuta ili maofisa wakutafutie waliokuibia na kukupiga.

Pia, unakumbuka polisi wenyewe hawatoki kituoni bure, na hawachukui Sh50 zako kwa kuwa wewe si dereva wa matatu, lazima utoboke donge nono!

Ghafla unakumbuka tangu mapema miaka ya 2000, polisi wametajwa kuwa watumishi wa umma ambao ni fisadi zaidi!

Hapo ndipo unapojipata ukijiuliza maswali ya kijinga: Kati ya polisi na wezi wanaojiita wachuuzi, nani hatari zaidi hivi kwamba anaweza kukutuma ‘zayuni’ kwa sekunde chache?

Unaingia baridi na kutamani kujikalia nyumbani badala ya kutoka nje ukutane na nuksi.

Kuishi Kenya, hasa Nairobi, kunapaswa kuwa tajriba ya kutosha kumpa mtu shahada ya kwanza ya chuo kikuu. Tunarushana kwa mazoea.

– Douglas Mutua ni Mkenya anayeishi Amerika (mutua_muema@yahoo.com)