Habari za Kitaifa

Kang’ata ajihusisha na Linda Mwananchi kwa mara ya kwanza baada ya kugura UDA

Na FATUMA BARIKI June 14th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

GAVANA wa Murang’a Irungu Kang’ata kwa mara ya kwanza amejihusisha na kundi la Linda Mwananchi wiki kadha baada ya kugura chama tawala cha UDA.

Katika hatua inayotarajiwa kuibua gumzo kuu la kisiasa, Gavana Kang’ata alijiunga na kundi hilo wakati wa mkutano uliofanyika Kivulini, Thika, Juni 14, 2026.

Katika hotuba yake, Bw Kang’ata alisema amependezwa na maono ya Linda Mwananchi akisema vuguvugu hilo limebeba sura ya Kenya ya viongozi wachanga wasioongozwa na ukabila.

Aliiponda serikali ya Rais Ruto akisema sera zake zimekuwa na athari mbaya kwa wafanyabiashara na wanaviwanda.

“Hii serikali inaongeza ushuru kampuni ambazo zinatupatia kazi mpaka zinaondoka Thika, zinaondoka Mt Kenya sababu ya gharama ya juu; na hivyo ndio vijana wanakosa kazi,” akasema Bw Kang’ata.

Alikosoa pia Ushuru wa Nyumba akisema fedha ambazo serikali inakusanya, alizosema zimefika Sh120 bilioni kufikia sasa, zingeelekezwa katika sekta ya elimu ili shule za kutwa ziwe bure kote nchini.

Alikashifu pia sera ya bima ya matibabu ya SHA akisema hospitali za Kaunti zinahangaika kutoa huduma kwa sababu serikali kupitia SHA hailipi madeni ya kusaidia huduma kuendelea.

Aliwataka viongozi wa Linda Mwananchi, Edwin Sifuna na Babu Owino wamtafute aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua ili kuunda upinzani thabiti utakaoweza kumng’oa Ruto mamlakani.