Jinsi muhogo mpya unaostahimili virusi unavyozalishwa
MUHOGO mpya unaostahimili magonjwa ya Cassava Brown Streak Disease (CBSD) na Cassava Mosaic Disease (CMD) umekuwa ukifanyiwa ukaguzi na utafiti wa kisayansi kwa zaidi ya miaka kumi.
Watafiti wa Shirika la Utafiti wa Kilimo na Maendeleo ya Mifugo Kenya (Kalro) kwa ushirikiano na wadau mbalimbali wa kimataifa, wamekuwa wakiufanyia majarabio dhidi ya magonjwa hayo.
Kulingana na Julia Njagi, Naibu Mkurugenzi anayesimamia utoaji leseni, ufuatiliaji na usimamizi wa usalama wa viumbe katika National Biosafety Authority (NBA), watafiti walitumia mbinu za bioteknolojia kuwezesha mmea kujikinga dhidi ya virusi vinavyosababisha magonjwa hayo.
“Lengo halikuwa kubadilisha sifa za muhogo kama chakula, bali kuuwezesha kupambana na virusi ambavyo husababisha hasara kubwa kwa wakulima,” anasema.

Baada ya maboresho hayo kufanyika kwenye maabara, miche ya muhogo ilipandwa katika maeneo maalumu ya majaribio yaliyodhibitiwa ili kutathmini usalama na uwezo wake wa kustahimili magonjwa.
Majaribio hayo yalifanyika katika vituo mbalimbali nchini ikiwemo Kalro Kandara, Mtwapa, Alupe, Kakamega na Kiboko.
Katika kila hatua, Julia anaelezea kwamba wataalamu walifuatilia ukuaji wa mimea, uwezo wake wa kuhimili virusi, kiwango cha uzalishaji na athari zozote zinazoweza kujitokeza kwa mazingira au watumiaji.
Beatrice Wambui, ambaye amekuwa akifanya kazi na mradi wa Virus Resistant Cassava for Africa (ViRCA) Plus tangu mwaka 2015, anasema uzalishaji wa mbegu za kupanda huanza kwa kuchagua mimea bora zaidi.
“Vipando hutolewa kutoka kwenye mimea yenye afya nzuri na kusambazwa kwa ajili ya kuzalishwa zaidi ili kuhakikisha wakulima wanapata mbegu safi na zenye ubora,” anasema.

Muhogo hupandwa kwa kutumia vipande vya shina vyenye urefu wa sentimita 20 hadi 30.
Aidha, vipando hivyo huwekwa kwenye udongo wenye rutuba na unyevunyevu wa kutosha, Wambui anasema. Kama aina nyingine za muhogo, muhogo huu mpya huhitaji palizi za mara kwa mara katika miezi ya mwanzo kabla ya kuanza kukua kwa kasi.
Kulingana na watafiti, tofauti kubwa ni kwamba aina hii ya muhogo ina uwezo wa kujikinga dhidi ya virusi vinavyosababisha magonjwa makuu ya muhogo, hivyo kuongeza nafasi ya wakulima kupata mavuno bora na tele.