Habari

Maraga sasa adai Rais Ruto anaendeleza ufisadi nchini

Na RUTH MBULA April 20th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

MWANIAJI wa urais David Maraga ameshambulia utawala wa Rais William Ruto akisema umezamia ufisadi ambao umesababisha nchi kupitia changamoto mbalimbali ambazo zingeweza kuzuiliwa.

Jaji huyo mkuu wa zamani alisema ni kinaya kuwa wale ambao wanafilisi nchi ndio wale wale ambao wamepewa jukumu la kuendesha masuala ya nchi.

“Ni kama kuwa na mchungaji wa mifugo wako kisha anakuibia. Hiyo iko wazi kabisa na tunazungumzia kinachofanyika,” akasema Bw Maraga akitaja mfano wa uhaba wa mafuta unaoshuhudiwa kati ya changamoto ambazo zimesababishwa na ufisadi.

Mwaniaji huyo wa urais wa UGM alikuwa akiongea wakati wa mazishi ya Mama Rose Nyabate Ontomwa, mamake mwanahabari wa KTN Francis Ontomwa.

“Mmeona sakata ya mafuta ambayo yamechangia kupanda kwa bei na mnafahamu jinsi bei ilivyopandishwa. Rais Ruto alisema atayaleta mafuta nchini kupitia makubaliano ya serikali na serikali,” akasema Bw Maraga.

Alishangaa kwa nini Shirika la ya Mafuta nchini (NOC) limetelekezwa katika uagizaji wa mafuta ilhali katika mataifa mengine, mashirika ya serikali ndiyo husimamia uagizaji wa mafuta.

Bw Maraga alisema kuwa anasaka urais kuhakikisha kuwa kila mtu anafuata sheria na yuko tayari kupambana na wafisadi.

“Hakuna afisa wa ngazi ya juu ya serikali ambaye atashiriki ufisadi na kuhepa kuadhibiwa. Nitakuwa wa kwanza kufuata sheria nikiwa rais na kila mtu atafuata jinsi ninavyofanya,” akasema Bw Maraga.

“Nimesafiri mataifa mengi ulimwenguni na tuna nchi nzuri ila hatua tunazostahili kuzipiga zimelemazwa na ufisadi,”

Bw Maraga alisisitiza kuwa licha ya kukosolewa kwa kuingilia siasa na yeye ni mzee wa kanisa, ataendelea kupambania haki kwa sababu watenda maovu wakiwa uongozini, watu hulia.

Kuhusu siasa za eneo la Gusii, alikashifu serikali kuhusu kifo cha mzee wa miaka 100 aliyeaga dunia Egetuki eneobunge la Bomachoge.

“Damu yam zee huyo ipo mikononi mwa Rais mwenyewe kwa sababu utawala wake ndio umewageuza watu kuwa ombaomba,” akasema Bw Maraga.