Habari

Gachagua, Matiang’i kung’ang’ania kiti cha eneobunge la Ol Kalou

Na CECIL ODONGO April 20th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

SIASA za ngome ambazo zimekuwa zikizua utata ODM sasa zimehamia upinzani huku mirengo miwili ikilaumiana kuhusu uchaguzi mdogo wa Ol Kalou.

Hata kabla ya Spika wa Bunge la Kitaifa Moses Wetangúla kutangaza kuwa kiti hicho ki wazi, taharuki ya kisiasa tayari imetanda huku Jubilee na DCP zikipambana kudhibiti siasa za eneobunge hilo.

Kiti cha eneobunge la Ol Kalou kilisalia wazi kutokana kifo cha mbunge wao David Kiaraho mnamo Machi 9.

Waziri wa zamani na mwanasiasa wa DCP Maina Kamanda kwenye mahojiano na Taifa Dijitali alisema upinzani haufai kufanya kosa na kuunga mkono Jubilee aliyosema si chama maarufu Ol Kalou bali pia Kaunti ya Nyandarua.

“Kushinda kiti hiki ni muhimu kwa sababu kutapitisha ujumbe wa kuhudumu kwa muhula mmoja kwa Rais Ruto. Kufanikisha hilo ni kupitia kumuunga mkono mgombeaji wa DCP,” akasema Mwanasiasa huyo mkongwe.

Bw Kamanda anasema kuwa walipoteza kiti cha ubunge wa Mbeere Kaskazini kwa sababu Kiongozi wa DP Justin Muturi aliwaongoza kuunga mkono mwaniaji na chama ambacho si maarufu.

“Iwapo wanaamini kuwa DCP si maarufu hapa Nyandarua na Ol Kalou basi wafanye utafiti wa kisayansi. Pia wakumbuke kuwa DCP ilishinda udiwani Kariobangi na Narok wakati Jubilee ilikuwa na wagombeaji,’ akaongeza mbunge huyo wa zamani wa Starehe.

Bw Kamanda ambaye ni mwandani wa aliyekuwa Naibu rais Rigathi Gachagua alidai kuwa marehemu Bw Kariaho alikuwa tu Jubilee kwa mwili lakini moyoni alikuwa akishabikia UDA.

“Hakuwa akihudhuria mikutano ya Jubilee na ni wazi alikuwa na ukuruba na UDA. Mbona sasa tuunge Jubilee ambayo mbunge wao alikuwa akifanya kazi na UDA?” akauliza Bw Kamanda akisisitiza DCP kimekita mizizi Ol Kalou.

Hata hivyo, Naibu Kiongozi wa Jubilee Jeremiah Kioni anasisitiza kuwa chama cha Jubilee hakitawaachia chama chochote kiti hicho.

“Tuna makubalino kwenye upinzani kuwa tutakuwa na mwaniaji kwenye uchaguzi mdogo unaokuja. Makubaliano yetu ni kuwa iwapo chama kilikuwa kikishikilia kiti na kisalie wazi, basi kitaungwa mkono na vyama vingine tanzu,” akasema Bw Kioni wiki jana huku akikanusha kuwa Jubilee kitawachia DCP kiti hicho.

Hata hivyo, Bw Kamanda ameshutumu Bw Kioni akidai ni fuko ndani ya upinzani na matamshi yake ya kisiasa hayafai kuchukuliwa kwa uzito.

“Anapiga kelele ili kuyumbisha upunzani ilhali anadai yeye ni mmoja wetu,” akasema Bw Kamanda.

Kwa mujibu wa mchanganuzi wa masuala ya kisiasa Profesa Masibo Munala, kuishinda Ol Kalou ndiko kutaonyesha Bw Gachagua ana uungwaji mkono Mlima Kenya.

“Jubilee inataka kujififua lakini ukweli ni kuwa DCP inaonekana ina umaarufu eneo hilo na kiongozi wake anachangamkiwa,” akasema Profesa Munala.
“Uhuru Kenyatta, Fred Matiang’I, Rigathi Gachagua na vinara wengine wapinzani wanahitaji kushirikiana ili washinde Ol Kalou,” akaongeza.
Mchanganuzi huyo anasema Jubilee ndiyo ipo pabaya kwa sababu wakiwasilisha mwaniaji na washindwe na DCP basi litakuwa ni pigo kuu kwao.