Dimba

Man City kuangusha ‘ndovu’ Arsenal juu ya meza ikiizaba Burnley EPL

Na MASHIRIKA April 22nd, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MANCHESTER City wana nafasi ya kupanda kileleni mwa jedwali la Ligi Kuu ya Uingereza (EPL), na wakati huohuo kuwashusha daraja Burnley iwapo watashinda mechi yao ya leo katika uwanja wa Turf Moor.

City, wanaotoka kupata ushindi muhimu wa 2-1 dhidi ya vinara Arsenal wikendi iliyopita, waliwahi kuwacharaza Burnley mabao 5-1 katika mechi ya mkondo wa kwanza, ambapo Erling Haaland alifunga mabao mawili huku mabao mawili ya kujifunga yakitoka kwa Maxime Esteve.

Baada ya ushindi dhidi ya Arsenal City ya Pep Guardiola wamechukua usukani wa mbio za ubingwa.

Tangu mwaka 2021, City hawajapoteza mechi ya ligi mwezi Aprili, jambo linaloonyesha uimara wao mwishoni mwa msimu.

Kwa sasa wako nyuma ya Arsenal kwa alama tatu lakini wana mechi moja mkononi, na wamekusanya alama nyingi zaidi ugenini tangu Desemba kuliko timu nyingine yoyote ya ligi.

Aidha, rekodi yao dhidi ya Burnley ni bora, wakiwa wameshinda mechi 14 kati ya 15 za mwisho za ligi dhidi yao.

Kwa upande wa Burnley, mambo ni magumu. Kikosi hicho kinachonolewa na Scott Parker kilichapwa 4-1 na Nottingham Forest wikendi iliyopita, na sasa kiko hatarini kushuka daraja kwa mara nyingine.

Kushuka kwao kunaweza kuthibitishwa iwapo West Ham United hawatapoteza mechi yao na Crystal Palace na Burnley wapoteze dhidi ya City.

Burnley wameshinda mechi moja tu kati ya 24 zilizopita za ligi na hawajapata ushindi wowote katika mechi 12 za nyumbani mfululizo.

Aidha, wamepoteza mechi 11 mfululizo dhidi ya City rekodi yao mbaya zaidi dhidi ya mpinzani yeyote.

Kwa upande wa vikosi, Burnley watawakosa Josh Cullen, Zeki Amdouni, Hannibal Mejbri, Jordan Beyer na Connor Roberts kutokana na majeraha, huku Axel Tuanzebe akifanyiwa tathmini kabla ya mechi ya leo.

City nao watamkosa Josko Gvardiol, huku Ruben Dias na Rodrigo Hernández wakiwa bado hawajulikani ikiwa watapatikana.

Endapo Rodri hatakuwa, Nico Gonzalez anaweza kuchukua nafasi yake. Nahodha Bernardo Silva pamoja na Rayan Cherki wanatarajiwa kuanza baada ya kung’ara dhidi ya Arsenal.

Mshambuliaji Haaland, ambaye ana wastani wa kufunga bao kila dakika 36 dhidi ya Burnley, anatarajiwa kuongoza safu ya ushambuliaji akisaidiwa na Jeremy Doku na Antoine Semenyo pembeni.

Katika mechi nyingine ya EPL, Bournemouth itawaalika Leeds United katika Uwanja wa Vitality usiku leo.

Bournemouth wanapania kufuzu michuano ya Europa msimu ujao wakipata ushindi nao Leeds United watakuwa wanapambana kujinasua kutoka hatari ya kushuka daraja.

Mara ya mwisho timu hizi kukutana katika Uwanjani Elland Road, mechi hiyo ikiishia sare ya 2-2, ambapo Eli Junior Kroupi alilazimisha sare baada ya kuifungia Bournemouth dakika za majeruhi.

Ratiba ya mechi za Jumatano, Aprili 22:

Burnley Vs Manchester City (10:00 pm)
Bournemouth Vs Leeds (10:00 pm)