Habari za Kaunti

Wakazi South C waandamana kuhusu jengo lililowaua watu wawili

Na KEVIN CHERUIYOT April 22nd, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MAMIA ya wakazi wa South C waliandamana barabarani  na kuzima shughuli za kibiashara huku wakitaka kukamatwa kwa wanaohusishwa na kuporomoka kwa jengo la ghorofa 16.

Wakati wa maandamano hayo ya amani, wakazi walisema kuwa miezi kadhaa imepita tangu tukio hilo lililosababisha vifo vya watu wawili na kuvuruga shughuli za eneo hilo, lakini hadi sasa hakuna mtu aliyekamatwa.

Maandamano hayo yaliwashirikisha wanajamii, viongozi wa eneo na wanaharakati waliotaka uwajibikaji na utekelezaji wa sheria za ujenzi.

Wakizungumza na wanahabari, wakazi hao walitoa muda wa siku saba kwa serikali kushughulikia masuala kadhaa waliyoeleza kuwa ni muhimu kwa usalama wa maisha na biashara zao katika eneo hilo.

Miongoni mwa madai yao ni kuchapishwa kwa ripoti ya uchunguzi wa mashirika mbalimbali ambayo serikali iliahidi kuitoa.

Walimtaka Waziri wa Ardhi na Makazi Alice Wahome, kutoa mara moja matokeo ya uchunguzi wa jengo lililoporomoka lililokuwa katika Barabara ya Muhoho kwenye ploti nambari 68/1306.

Pia wakazi walitaka ripoti ya hali ya jengo la Bridge Port (LR No. 209/5909/9) lililo karibu na jengo lililoporomoka.

“Tunahitaji uthibitisho wa usalama wa umma au amri ya kubomolewa kwa jengo la ghorofa 15 linalomilikiwa na Bridge Port. Jengo hili liliidhinishwa kuwa na ghorofa 10 lakini sasa lina 15, huku nguzo zake zikiwa na uharibifu wa kimuundo,” wakasema.

Aidha walitaka maafisa waliokuwa wazembe kufunguliwa mashtaka.

“Tunahitaji majina ya maafisa wa Kaunti ya Nairobi na Mamlaka ya Kitaifa ya  Ujenzi (NCA)  ambao walishindwa kuchukua hatua kufuatia notisi tatu za utekelezaji zilizotolewa mnamo 2025. Uzembe ni kosa la jinai, na ni wakati wa kuwawajibisha watu binafsi, si taasisi pekee,” waliongeza.

Aidha, waliitaka serikali kuwaorodhesha watengenezaji na wataalamu wasiofuata sheria katika jiji, na kuweka wazi majina ya waliohusika katika miradi iliyofutwa na kuzuiwa kuendelea na ujenzi nchini.

“Tunahitaji pia taarifa ya kina kuhusu ukaguzi wa majengo. Waziri Wahome aliahidi ukaguzi wa kufuata sheria ili kuzuia majanga kama haya. Tunataka kujua ni majengo mangapi yamekaguliwa tangu Januari 2026 na ni mangapi yaliyo hatarini yameondolewa watu,”