Habari za Kaunti

Kuuawa kwa kijana kwa kupigwa risasi na polisi kwazua hasira na maandamano Garissa

Na MANASE OTSIALO April 23rd, 2026 Kusoma ni dakika: 1

TAHARUKI ilitanda katika mji wa Garissa baada ya wakazi kuandamana kulalamikia walichotaja kuwa ukatili wa polisi kufuatia kifo cha kijana mmoja dereva, Aden Mohamed Hassan.

Hassan anaripotiwa kupigwa risasi na polisi katika eneo la Modika alipofika kumsaidia rafiki yake aliyekuwa amekamatwa.

Kwa mujibu wa rafiki huyo, Abdi Mohamud, polisi walivamia gari lake na kulifyatulia risasi kabla ya kumkamata.

“Alipofika tu alipigwa risasi kwenye paji la uso,” alisema Mohamud, akikanusha kuhusika na magendo ya sukari kutoka Somalia.

Kifo hicho kilichochea hasira, huku wakazi wakichukua mwili katika mochari ya Hospitali ya Rufaa ya kaunti ya Garissa na kuandamana hadi kituo cha polisi wakitaka haki.

Polisi walitumia vitoa machozi kuwatawanya.

Mwakilishi wa Wanawake wa Garissa Udgoon Siad, alikemea mauaji hayo akisema washukiwa wanapaswa kufikishwa mahakamani badala ya kuuawa.

Kamanda wa polisi wa eneo hilo, John Nzioka, alithibitisha tukio hilo na kusema uchunguzi unaendelea kwa ushirikiano na Mamlaka Huru ya Kuchunguza Utendakazi wa Polisi (IPOA).