Habari za Kitaifa

Agizo la Wetang’ula kuhusu vitambulisho laibua ubishi mkali

Na MOSES NYAMORI April 23rd, 2026 Kusoma ni dakika: 2

AGIZO la Spika wa Bunge la Kitaifa, Moses Wetang’ula kwa wabunge kuwatumia wafanyakazi wao kuchukua na kusambaza vitambulisho vya kitaifa limeibua mjadala mkali kuhusu usalama wa taifa na uwezekano wa kuingiza siasa katika utoaji wa huduma za umma.

Wakosoaji wametaja agizo hilo kuwa hatari na lisilo na uwajibikaji, wakionya kuwa stakabadhi hizo muhimu zinaweza kuishia mikononi mwa watu wasiofaa, hali inayoweza kuhatarisha usalama wa nchi.

Aidha, wanasema hatua hiyo inaweza kuathiri uadilifu wa mchakato wa kusajili wapigakura, hasa ikizingatiwa kuwa wabunge wana maslahi ya moja kwa moja katika matokeo ya uchaguzi.

Akizungumza bungeni mnamo Jumanne, Bw Wetang’ula aliwataka wabunge kuchukua jukumu kubwa zaidi katika kuhakikisha vitambulisho vinawafikia wanaoomba kuvipata.

Alisema ni wajibu wao kutumia wafanyakazi walio katika ofisi za maeneo yao kusaidia kusambaza vitambulisho hivyo.

“Tunalia kwamba hakuna vitambulisho, lakini vinapotolewa havichukuliwi. Vinabaki katika ofisi za wasimamizi wa maeneo na machifu,” alisema Spika, akiwahimiza wabunge kushirikiana na maafisa wa serikali kutambua waombaji na kuhakikisha wanapata vitambulisho vyao kwa wakati.

Agizo hilo lilitolewa kutokana na hoja ya Mbunge wa Mandera Kusini, Abdul Haro, aliyelalamikia ucheleweshaji wa utoaji wa vitambulisho katika eneo lake.

Alisema hali hiyo inaweza kuwanyima maelfu ya vijana haki yao ya kujisajili kupiga kura.

Hata hivyo, wadau wa sheria na utawala bora wameonya kuwa hatua hiyo inaweza kufungua mianya ya matumizi mabaya ya mamlaka.

Rais wa Chama cha Wanasheria Kenya (LSK), Charles Kanjama, alisema mchakato wa utoaji wa vitambulisho unapaswa kusimamiwa kikamilifu na serikali kupitia mifumo rasmi iliyowekwa.

“Ni jambo lisilo la kawaida. Wanaoomba kupata vitambulisho wanapaswa kuvichukua wenyewe kwa kufuata taratibu zilizopo, ikiwemo kuthibitisha ni vyao. Kuruhusu watu wengine kuhusika ni hatari na kunaweza kusababisha stakabadhi hizi kuishia mikononi mwa watu wasiofaa,” alisema Kanjama.

Mkurugenzi Mtendaji wa Kituo cha Demokrasia ya Vyama Vingi (CMD-Kenya) Frankline Mukwanja, alisema kushiriki kwa wabunge katika utekelezaji wa shughuli hiyo kunaweza kuchanganya mipaka kati ya huduma za umma na siasa za ushindani.

Alionya kuwa hali hiyo inaweza kusababisha upendeleo katika usambazaji wa vitambulisho, ambapo maeneo yanayoonekana kuunga mkono wabunge fulani yanaweza kupewa kipaumbele, huku mengine yakipuuzwa.

“Wabunge si wadau huru; wana maslahi ya kisiasa. Kushiriki kwao moja kwa moja kunaweza kuleta mgongano wa maslahi katika mchakato unaoathiri uchaguzi wenyewe,” alisema Mukwanja.

Aidha, alibainisha kuwa ikiwa wananchi wataanza kuamini kuwa kupata vitambulisho au kujisajili kupiga kura kunategemea uhusiano wa kisiasa, imani kwa taasisi muhimu kama Tume ya Uchaguzi (IEBC) inaweza kudhoofika kwa kiasi kikubwa.

Katika Bunge la Kitaifa, wabunge kadhaa waliibua wasiwasi kuhusu ucheleweshaji wa utoaji wa vitambulisho.

Mbunge wa Funyula, Wilberforce Oundo, alisema muda uliowekwa rasmi wa siku tatu hadi saba hauzingatiwi, akibainisha kuwa baadhi ya wanaoomba kuzipata stakabadhi hizo wamekuwa wakisubiri kwa miezi minne au zaidi.

“Wapo waliotuma maombi tangu Agosti na Septemba mwaka jana lakini bado hawajapata vitambulisho vyao,” alisema Oundo.

Naye Mbunge wa Kajiado Kaskazini, Onesmus Ngogoyo, alitaka serikali kuchukua hatua za haraka kuhakikisha wale ambao vitambulisho vyao viko tayari wanaitwa kuvichukua ili waweze kushiriki katika usajili wa wapigakura.

Mjadala huu unaangazia changamoto kubwa katika utoaji wa huduma za umma nchini, ambapo masuala ya kiutawala, usalama na siasa yanaingiliana.

Huku serikali ikijaribu kuongeza ufanisi katika utoaji wa vitambulisho, wadau wanasisitiza umuhimu wa kulinda uadilifu wa mchakato huo ili kuhakikisha haki, usawa na imani ya umma vinadumishwa.