Mabadiliko ya maafisa wa kaunti wazua mjadala
DIWANI wa Nairobi South ambaye pia ni Naibu Kiongozi wa Wachache katika Bunge la Kaunti ya Nairobi, Waithera Chege, amempa Gavana Johnson Sakaja saa 24 kufuta mabadiliko ya maafisa wakuu wa kaunti yaliyotangazwa Ijumaa Aprili 24, 2026 akidai yanaibua maswali kuhusu uwazi katika idara ya ardhi.
Bi Chege alipinga kuhamishwa kwa Cecilia Koigu kutoka Idara ya Ardhi hadi ICT na nafasi yake kuchukuliwa na Dkt Machel Waikenda, ambaye awali alikuwa akisimamia sekta ya Miundomsingi na ICT.
Kwa mujibu wa waraka kutoka Afisi ya Gavana, NCC/ADM/GOV/063/2026, mabadiliko hayo yalifanywa chini ya Kifungu cha 45(5) cha Sheria ya Serikali za Kaunti ya 2012 na yanaanza kutekelezwa mara moja.
Lakini Bi Chege alieleza kuwa mabadiliko hayo ni ya kutatanisha na yanaweza kudhoofisha usimamizi wa ardhi jijini, akisisitiza kuwa idara hiyo ni muhimu katika mipango ya miji, utoaji wa idhini za ujenzi na utekelezaji wa sheria.

“Idara ya ardhi si uwanja wa majaribio ya kisiasa. Mabadiliko ya ghafla bila maelezo yanaweza kuhatarisha mfumo wa usimamizi wa ardhi,” alisema.
Alidai hatua hiyo inaweza kuvuruga kumbukumbu za taasisi na kudhoofisha juhudi za kukabiliana na ujenzi haramu na changamoto za makazi duni.
Bi Chege alionya kuwa iwapo Gavana Sakaja hatarejesha Bi Koigu katika wadhifa wake ndani ya saa 24, Bunge la Kaunti litachukua hatua kali za usimamizi dhidi ya serikali ya kaunti.
Aidha, alidokeza huenda kuna maslahi fiche yanayohusishwa na mabadiliko hayo, madai yaliyozidisha mjadala kuhusu uwajibikaji katika sekta ya ardhi ambayo kwa muda mrefu imekumbwa na migogoro.
Hata hivyo, wandani wa Gavana Sakaja wanatetea hatua hiyo wakisema kupanga upya maafisa ni mamlaka yake ya kikatiba.