Habari

Huzuni watu 7 wakiuawa katika ghasia za mpakani Kitui

Na PIUS MAUNDU April 27th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

TAHARUKI imetanda katika eneo la Tseikuru, Kaunti ya Kitui baada ya wachungaji wa ngamia kuwaua watu saba.
Kamanda wa Polisi wa Tseikuru, Mecha Mogeni alithibitisha uvamizi huo ambao ulifanyika katika Kituo cha Kibiashara cha Kwa Kamari kwenye barabara ya Mwingi-Tseikuru mnamo Jumamosi jioni.
“Wavamizi walifika kwenye soko la Kwa Kamari na kuanza kuwapiga watu risasi. Waliwaua watu watatu sokoni kisha wakawaua wengine kwenye Mbuga ya Wanyama ya Mwingi,” akasema Bw Mogeni.
“Mwanaume ambaye alipigwa risasi bado anaendelea kuuguza majeraha katika Hospitali ya Kaunti-ndogo ya Tseikuru.
“Tunaendelea kuwaandama waliohusika na uvamizi huo,” akaongeza.
Wale ambao waliuawa ni mwanamke na wanaume sita.
Walioshuhudia kisa hicho walisema wavamizi hao waliyateketeza maduka, vituo vya mafuta na pikipiki.
Hali ilipotulia ndipo watu watatu walibainika wamekufa huku ikibainika wavamizi hao walikuwa wakiendeleza mauaji walipokuwa wakitoka sokoni.
Madhumuni ya uvamizi huo bado hayajajulikana.
Hata hivyo, polisi wanaamini ni uvamizi wa kulipiza kisasi baada ya watu wasiojulikana kumuua mchungaji wa ngamia eneo hilo.
Tseikuru imekuwa kitovu cha vita kati ya wakulima na wachungaji ngamia, pande hizo mbili zikizozania maji na nyasi.
Tukio la hivi punde linaongeza idadi ya watu ambao wameuawa kwenye matukio kama hayo hadi watu 14.
Eneo hilo huwa ni mpaka wa kaunti za Kitui na Tana River.
“Hivi ni vifo vingi katika eneo moja na tunaendelea kuwaandama wachungaji hao wa ngamia ambao walivamia mbuga ya wanyamapori ya Mwingi,” akasema Kamishina wa Kitui, Erastus Mbui.
 “Tumewatuma polisi wa kawaida na wale wa kupambana na fujo maarufu kama GSU kuwaandama wale waliotekeleza mauaji hayo na pia kuhakikisha kuna utulivu,” akasema Bw Mbui.