Habari za Kaunti

Shahidi afichua mazishi ya kinyama Kwa Binzaro, ya miili kuachwa kuliwa na wanyama porini

Na BRIAN OCHARO April 29th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

KESI ya mhubiri Paul Mackenzie na Sharleen Temba Anindo ya uhalifu dhidi ya binadamu kuhusu vifo Kwa Bi Nzaro imeanza Mombasa, ikiashiria hatua ya kihistoria katika mfumo wa haki nchini.

Hii ni mara ya kwanza kwa Kenya kutumia sheria hizo za Mkataba wa Roma zinazosimamia Mahakama ya Kimataifa Kuhusu Uhalifu (ICC), katika kesi inayoendelezwa ndani ya nchi.

Katika siku ya kwanza ya kesi, mpelelezi aliyeshiriki katika zoezi la kufukua miili ya waathiriwa Kwa Bi Nzaro, Kaunti ya Kilifi, alieleza kwa kina jinsi miili ilivyofichwa kimakusudi, kuliwa na wanyama wa porini na kusambazwa kila mahali ndani ya msitu huo.

Ushahidi wa Inspekta wa polisi Timothy Bett, ulieleza kuwa, wachunguzi walifukua miili 30 kutoka makaburi 19, lakini pia walipata sehemu 102 za miili zilizokuwa zimetawanyika msituni.

Uchunguzi wa kitaalamu wa miili ulionyesha kuwa jumla ya waathiriwa ilikuwa 52.

Mackenzie na Anindo almaarufu kama Ann, wameshtakiwa pamoja na Kahindi Kazungu Garama almaarufu Mlewa, Tom Ochieng Mkonwe almaarufu Thomas au Tomaso, Julius Tuva Luwali, Johnson Gona Richard, Charles Mutua Musee almaarufu Mzee Mutua na James Kazungu Kahindi almaarufu Ponda au Baba Bura.

Wanane hao wameshtakiwa kwa makosa 23 yanayohusiana na vifo vya watu 52 katika msitu huo kati ya Januari na Oktoba 2025. Wote walikanusha mashtaka.

“Miili mingi ilikuwa uchi. Ilizikwa katika makaburi ya kina kifupi kisichozidi futi mbili ili kuharakisha kuoza na kuruhusu wanyama kuifikia. Hili lililenga kuficha ushahidi wa vifo katika eneo hilo,” Bett aliiambia mahakama.

Alieleza kuwa, mabaki mengi yalipatikana nje ya makaburi, mifupa ikiwa imetengana na kutapakaa mbali na makaburi.

Aidha, alisema makaburi kadhaa yalifichwa kwa makusudi ndani ya kichaka na kufunikwa kwa matawi yenye miba ili yasigunduliwe kwa urahisi.

Bw Bett alibainisha tofauti kubwa kati ya mbinu za mazishi Shakahola na Kwa Bi Nzaro, akisema eneo hilo lilionyesha mpango mahsusi wa kuficha ushahidi.

Wakati waathiriwa wa awali walizikwa katika makaburi ya pamoja karibu na makazi yao, wale wa Kwa Bi Nzaro walizikwa takriban mita 500 kutoka makazi yaliyotumika kama kituo cha kufunga.

“Kaburi la kwanza lilipatikana mita 500 kutoka makazi hayo. Hili halikuwa la bahati mbaya bali mpango uliopangwa kwa makini kuficha ushahidi wa vifo,” alisema.

Nguo za waathiriwa zilichomwa moto au kuzikwa karibu na majengo yaliyotumika kwa shughuli za kufunga.

Kati ya miili 52 iliyopatikana, ni miwili pekee iliyokuwa katika hali inayoruhusu uchunguzi kamili wa maiti, yote ikiwa na majeraha ya kichwa yaliyosababishwa na kipigo kizito.

Miili mingine 50 ilikuwa imeoza kiasi cha kutoruhusu kubainika kwa chanzo cha vifo.

Awali, mtaalamu wa usoroveya Michael Mwania, aliiambia mahakama kuwa Kwa Bi Nzaro iko takriban kilomita nne kutoka msitu wa Shakahola, jambo linalounganisha maeneo hayo mawili muhimu katika kesi hiyo.

Hata hivyo, washtakiwa kupitia wakili wao wamepinga kesi hiyo, wakitaka mahakama kuchunguza kwa kina namna upande wa mashtaka unavyokusudia kuwasilisha na kuthibitisha ushahidi wake.

“Iweje mtu aliye chini ya ulinzi wa serikali aweze kupanga na kusababisha vifo vya watu 52 akiwa ndani ya gereza lenye ulinzi mkali?” alihoji wakili.