Siasa

Kindiki, Gachagua na Matiang’i sasa kupimana nguvu uchaguzini Ol Kalou

Na MWANGI MUIRURI April 29th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

UCHAGUZI mdogo wa eneobunge la Ol Kalou unaonekana kama kipimo kikuu cha mwelekeo wa kisiasa wa ukanda wa Mlima Kenya kuelekea Uchaguzi Mkuu wa 2027.

Uchaguzi huo utakaofanyika Julai 16, 2026, unatazamiwa kuamua upande ulio na nguvu halisi kati ya serikali na upinzani katika eneo hilo muhimu kisiasa.

Vita hiyo vya kisiasa vitawakutanisha Naibu Rais Kithure Kindiki, aliyeteuliwa kuongoza kampeni za chama tawala cha United Democratic Alliance (UDA), mtangulizi wake Rigathi Gachagua kupitia chama chake kipya cha Democracy for Citizens Party (DCP), pamoja na kiongozi wa Chama cha Jubilee, Fred Matiang’i.

Bw Gachagua ameutaja uchaguzi huo kama “kura ya maoni” kuhusu mustakabali wa Mlima Kenya, akisisitiza kuwa hakuna chama kinachopaswa kuachia wapinzani ngome yake.

Kauli yake imeongeza joto la kisiasa katika eneo ambalo tayari lina ushindani mkali.

Kiti cha eneo bunge la Ol Kalou, lililopo Kaunti ya Nyandarua, kilitangazwa wazi kufuatia kifo cha mbunge David Kiaraho mnamo Machi 29, 2026 akiwa na umri wa miaka 63.

Bw Kiaraho alikuwa akihudumu kwa muhula wa tatu baada ya kushinda uchaguzi kwa tiketi ya Jubilee.

Katika uchaguzi uliopita, Bw Kiaraho alipata kura 24,058, akimshinda mpinzani wake wa UDA Kamau Ngotho aliyepata kura 19,380, ishara ya ushindani mkali unaotarajiwa kujirudia tena.

Baada ya kuvuliwa wadhifa wa Naibu Rais mwaka 2024, Bw Gachagua alianzisha DCP na kujisawiri kama msemaji wa kisiasa wa ukanda wa Mlima Kenya.

Ameonyesha wazi kuwa atapigania kila nafasi kuhakikisha chama chake kinapata ushawishi mkubwa katika uchaguzi ujao.

DCP na Jubilee ni sehemu ya muungano wa upinzani hali inayozua mvutano mkubwa kati ya Bw Gachagua na Dkt Matiang’i, ambao wote wanamezea mate tiketi ya urais ya upinzani mwaka 2027.

Hii imeongeza mgawanyiko wa ndani unaoweza kuathiri mikakati yao ya pamoja.

Katika upande wa serikali, Profesa Kindiki ana jukumu zito la kuhakikisha UDA ya Rais William Ruto inaendelea kudhibiti Mlima Kenya, eneo ambalo lilimpa kiongozi wa nchi takriban asilimia 87 ya kura mwaka 2022. Kupoteza sehemu ya ushawishi huo kunaweza kubadilisha kabisa hesabu za 2027.

Wachambuzi wa siasa wanasema changamoto ya Prof Kindiki ni kubwa, hasa kutokana na mvutano wa Bw Gachagua ambaye ameweka wazi azma yake ya “kudhibiti kura za Mlima Kenya.”

Kwa upande wake, Prof Kindiki amemtaja Bw Gachagua kama kiongozi mwenye “ kujipiga kifua bila msingi,” akiahidi kushinda uchaguzi huo mdogo na kuthibitisha chama cha UDA kina nguvu katika ukanda huo.

Naibu Kiongozi wa Jubilee, Bw Jeremiah Kioni amesema kiti hicho kinapaswa kurejea kwa chama chake kama sehemu ya kuheshimu ushirikiano wa upinzani.

Hata hivyo, Bw Gachagua amepuuza wito huo, akisisitiza kuwa DCP itatoa mgombea wake na tayari ana orodha ya watu tisa wanaowania tiketi.

Prof Kindiki naye amedai kuwa UDA ina zaidi ya wagombea 10 walio katika mchakato wa uteuzi, akisema chama chake kiko tayari kwa mapambano ya moja kwa moja.

Uchaguzi mdogo uliopita wa Mbeere North umeendelea kutajwa kama mfano wa mgawanyiko wa upinzani, ambapo mgombea wa serikali alishinda kwa tofauti ndogo baada ya upinzani kugawanya kura.

Wachambuzi wanasema hali kama hiyo inaweza kujirudia Ol Kalou ikiwa makundi ya kisiasa hayatapata mwafaka.

Wanasiasa wakongwe kama Bw Maina Kamanda wanasema uchaguzi huo unapaswa kuwa wa wazi bila makubaliano ya kujiondoa kwa upande wowote, ili kupima nguvu halisi ya vyama.

Ol Kalou sasa imegeuka kuwa uwanja wa majaribio ya nguvu kati ya serikali na upinzani.

Matokeo yake hayatatoa tu mbunge mpya, bali pia yataonyesha nani anaweza kudhibiti mwelekeo wa Mlima Kenya kuelekea 2027.