JSC yamteua Warsame kuwa jaji katika Mahakama ya Juu
TUME ya Huduma ya Mahakama nchini (JSC) imemteua Jaji Mohammed Warsame kuwa Jaji wa Mahakama ya Juu.
Jaji Warsame wa Mahakama ya Rufaa aliteuliwa kujaza pengo lililoachwa kufuatia kifo cha Jaji Mohammed Ibrahim.
Sasa jina lake litapelekwa kwa Rais William Ruto kuapishwa kuanza kutekeleza majukumu yake.
Uteuzi wa Jaji Warsame umewadia wakati nchi inajitayarisha kufanya uchaguzi mkuu wa 2027.
Wakiongozwa na Jaji Mkuu Martha Koome, makamishna wa JSC walimteua Jaji Warsame baada ya kuwashinda majaji wenzake katika Mahakama ya Rufaa Katwa Kigen na Francis Tuiyott.
Wengine waliokuwa wameorodheshwa kuwania wadhifa huo ni pamoja na Jaji wa Mahakama Kuu Joseph Sergon na aliyekuwa mwenyekiti wa Mamlaka Huru ya usimamizi wa Polisi (IPOA) Anne Waceke Makori.
Jaji Warsame aliyeibuka kidedea amefikia kilele cha taaluma yake ya uanasheria na ujaji kwa kujiunga na Mahakama hii ya Upeo.
Makamishna wa JSC walikuwa wanamulika nidhamu ya utendakazi, ustawishaji sheria na uzoefu wa utendakazi katika idara ya mahakama kwa uangavu na uwazi.
JSC ilimteua Jaji huyu kwa vile alionyesha weledi katika kufafanua masuala ya sheria na ujuzi mpevu katika kusimamia na kudhibiti mahakama wakati wa kuendesha kesi.
Aidha, aliteuliwa kwa uadilifu na ujuzi wa miaka mingi katika idara ya mahakama.
Jaji Warsame alijiunga na idara ya mahakama 2003 baada ya kufanya kazi ya uwakili tangu 1994 alipohitimu kutoka chuo kikuu cha Nairobi.
Alipokuwa msimamizi wa kamati ya urekebishaji tabia ya idara ya mahakama Jaji Warsame alipendekeza kuachiliwa kwa wafungwa wa makosa madogo 7,000.