Ripoti ya KNBS: Murang’a ndio inapiga kasi zaidi katika ukuaji wa kiuchumi
KAUNTI ya Murang’a ndiyo inayokua kwa kasi zaidi eneo la Mlima Kenya katika nyanja ya uchumi ikiandikisha mchango thabiti kwa mapato ya jumla nchini (GDP), ripoti imeashiria.
Ripoti ya Shirika la Kitaifa kuhusu Takwimu Nchini (KNBS) iliashiria kuwa kaunti hiyo inayoongozwa na Gavana Irungu Kang’ata iliandikisha ukuaji wa zaidi ya asilimia 13 kiuchumi kati ya 2023 na 2024 pekee.
Ukuaji huo uliwezesha uchumi wa kaunti hiyo kufikia Sh295.89 bilioni baada ya kuandikisha ukuaji wa zaidi ya 34,000 uliopigwa jeki na shughuli anuai za kiuchumi na kilimo.
Ukuaji huo uliwezesha kaunti hiyo kupiku mshindani wake wa karibu, Kaunti ya Nyeri, kwa umbali wa karibu asilimia tano, kuashiria nafasi yake katika eneo la Mlima Kenya.
Japo ingali nyuma ya vigogo wa kiuchumi kama vile kaunti za Nakuru na Kiambu, ripoti hiyo iliashiria kuwa Murang’a kwa sasa inajivunia mchango wa tatu mkubwa zaidi kwa uchumi wa Kenya kutoka eneo hilo ikiwa na 295.89 bilioni zilizokuwa kutoka Sh261.52 bilioni.
Licha ya Nakuru kuwa kaunti ya tatu kubwa zaidi kuhusiana na mchango wake kwa uchumi nchini, iliandikisha kasi ya chini zaidi ya ukuaji kwa asilimia 2.1 pekee.
Murang’a iliipiku Nairobi kwa pointi sita ikipigwa jeki na utendakazi wake katika sekta za kilimo na utoaji huduma.
Embu ikiwa na ukuaji kwa kasi ya asilimia 8.3 inawakilisha kaunti ya tatu inayokua kwa kasi zaidi eneo la Mlima Kenya ikifuatiwa na Meru kwa asilimia nane, Kiambu, asilimia 7.7 na Kirinyaga, asilimia 7.1 percent.
Uchumi wa Nairobi unakadiriwa kuwa Sh4,105.6 bilioni ukifuatiwa na Kiambu Sh819.8 bilioni na Nakuru, Sh771.8 bilioni.
Ni kaunti tano pekee zilizoandikisha ukuaji kiuchumi kwa zaidi ya Sh500 bilioni zikiwemo Mombasa na Meru iliyopigwa jeki na matokeo thabiti katika sekta ya kilimo.
“Kaunti zenye vituo vikuu vya kibiashara ikiwemo Nairobi, Kiambu, Nakuru, Mombasa na Machakos ziliandikisha hisa za ziada zenye thamani ya juu kwa jumla huku kaunti zinazoongoza kwa kilimo na kiuchumi kama vile Meru, Kakamega, Nyeri na Murang’a vilevile zikichangia pakubwa,” ilisema ripoti.