Tabasamu Leba Dei Ruto ‘akipanga’ wafanyakazi
RAIS William Ruto Ijumaa, Mei 1, 2026 aliwapa wafanyakazi zawadi ya nyongeza ya mishahara ya asilimia 12 na asilimia 15 kwa walio katika sekta ya kilimo.
Kufuatia tangazo hilo katika sherehe za kihistoria za Siku ya Wafanyakazi (Leba Dei) zilizofanyika kwa mara ya kwanza nje ya jiji la Nairobi, mishahara ya chini kwa wafanyakazi inaongezeka hadi Sh4,363.31.
“Kwa kutambua kujitolea, ustahimilivu na mchango mkubwa wa wafanyakazi wetu katika ukuaji na uthabiti wa uchumi wetu, nina furaha kutangaza ongezeko la asilimia 12 ya mishahara ya jumla na asilimia 15 kwa sekta ya kilimo,” alisema Rais Ruto akiwa Vihiga.
Mabadiliko hayo yatakapotekelezwa yatawanufaisha wafanyakazi wa ngazi ya chini kama wasafishaji, wafagiaji, wafanyakazi wa nyumbani na walinzi wa mchana kwa kupata nyongeza kati ya Sh1,031.58 na Sh4,363.31.
Nchini Kenya, kiwango cha chini cha mshahara hutofautiana kulingana na sekta na eneo, na kinahusisha takribani makundi 45.
Nyongeza hiyo ni chini ya asilimia 23 iliyopendekezwa na Katibu Mkuu wa COTU-K Francis Atwoli, huku Shirikisho la Waajiri Kenya (FKE) likipinga na kupendekeza isizidi asilimia 5. Rais Ruto alionekana kuchukua msimamo wa kati.
Kundi litakalofaidika zaidi kwa kiwango kikubwa ni mafundi daraja la I, makarani wa fedha, madereva wa magari makubwa na wauzaji mijini kama Nairobi, Mombasa, Kisumu, Nakuru na Eldoret, ambapo mshahara utaongezeka hadi Sh40,724.23 kutoka Sh36,360.92.
Sekta ya kilimo itashuhudia ongezeko dogo zaidi kwa wafanyakazi wasio na ujuzi wakipata Sh1,200 zaidi kufikia Sh9,197 kwa mwezi, huku madereva wa malori na magari wakipata nyongeza ya mishara ya Sh1,758 hadi Sh13,477.
Hata hivyo, ongezeko hilo ni chini ya nusu ya pendekezo la asilimia 23 lililowasilishwa na Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi (COTU-K), jambo lililozua mjadala kuhusu iwapo sauti ya wafanyakazi inazingatiwa kikamilifu.
Rais Ruto aliwashukuru wafanyakazi kwa mchango wao katika kukuza uchumi, akisema nyongeza hiyo ni ishara ya kuthamini juhudi zao.
Alisisitiza kuwa uchumi wa Kenya unaendelea kuimarika licha ya changamoto za kimataifa, akitaja ukuaji wa Pato la Taifa kwa asilimia 4.6, kushuka kwa mfumuko wa bei hadi asilimia 5.6, na uthabiti wa shilingi kwa takribani Sh129 dhidi ya dola.
Rais alisema kuwa mpango wa nyumba za bei nafuu umeajiri zaidi ya watu 640,000, huku lengo likiwa kufikia ajira milioni moja.
Vijana wanachukua asilimia 50 ya nafasi hizo, wanawake asilimia 30 na watu wenye ulemavu asilimia 5.
Katika Kaunti ya Vihiga pekee, uwekezaji umefikia zaidi ya Sh15 bilioni, ukiwemo ujenzi wa nyumba 3,720 na soko lenye vibanda 3,470.
Kuhusu ajira nje ya nchi, Rais alisema zaidi ya Wakenya 580,000 wamepata kazi kupitia mpango wa “Kazi Majuu”, unaojumuisha sekta mbalimbali kama uhandisi, udereva, uuguzi na ualimu, kupitia makubaliano ya kimataifa.
Katika sekta ya miundombinu, alizungumzia upanuzi wa Barabara ya Rironi–Mau Summit akisema itazalisha ajira 10,000 moja kwa moja. Pia, alitaja reli ya Kisumu–Malaba ya kilomita 107 kama miongoni ya miradi itakayochochea uchumi wa Magharibi na Bonde la Ufa.
Akizungumzia bima ya afya chini ya Mamlaka ya Afya ya Jamii (SHA), Rais alikiri changamoto za awali lakini akasema zimeanza kushughulikiwa.
Aliongeza kuwa zaidi ya Wakenya milioni 30.8 sasa wamejiunga na mpango huo, ikilinganishwa na milioni 8 waliokuwa chini ya NHIF miaka mitatu iliyopita.
Rais pia alitangaza kuwa Kenya imekamilisha kuidhinisha mikataba ya Shirika la Kazi Duniani (ILO) nambari 189 na 190 kuhusu haki za wafanyakazi wa nyumbani na kuzuia unyanyasaji kazini.
Aliwataka Wakenya kupuuza taarifa za kupotosha, akisema: “Kelele zinaweza kusikika, lakini haziwezi kubadilisha ukweli. Ukweli wa taifa unaonekana katika matendo ya kila siku ya wananchi.”
Sherehe hiyo ilihudhuriwa na viongozi mbalimbali, akiwemo Mkuu wa Mawaziri Musalia Mudavi na Spika wa Bunge la Kitaifa Moses Wetang’ula.