Makala

Kuna mafuriko sasa lakini afueni yaja, idara yasema

Na BENSON MATHEKA May 1st, 2026 Kusoma ni dakika: 2

Wakenya huenda wakapata afueni hivi karibuni licha ya mvua kubwa inayoendelea kunyesha katika maeneo mbalimbali ya nchi, baada ya Idara ya Utabiri wa  Hali ya Hewa nchini kutangaza kuwa mvua hiyo inatarajiwa kupungua.

Kwa mujibu wa taarifa ya hali ya hewa iliyotolewa Ijumaa, Mei 1, mvua kubwa inayoshuhudiwa katika sehemu nyingi za nchi inatarajiwa kupungua kwa kiasi kikubwa kufikia katikati ya mwezi huu wa Mei 2026.

Idara hiyo ilieleza kuwa ingawa wiki ya kwanza ya Mei itaendelea kushuhudia mvua kubwa katika maeneo kadhaa, hali ya hewa inatarajiwa kuimarika katika nusu ya pili ya mwezi.

“Tathmini ya mwezi wa Mei inaonyesha kuwa nusu ya pili ya mwezi huenda ikawa kavu kuliko kawaida, ikimaanisha mwisho wa msimu wa mvua za Machi, Aprili na Mei 2026,” ilisema taarifa hiyo.

Hata hivyo, si maeneo yote yatapata afueni ya haraka kutokana na mvua. Maeneo kama vile Mlima Kenya, Magharibi mwa nchi, Bonde la Ziwa Victoria na Pwani yanatarajiwa kuendelea kupokea mvua hadi mwezi Juni, ingawa kiwango chake kitakuwa chini ya wastani.

Mwisho wa mvua hii ndefu utaashiria kuanza kwa msimu wa baridi na ukavu, ambapo baadhi ya maeneo hasa Nyanda za Juu yanatarajiwa kushuhudia baridi kali.

Licha ya matarajio ya kupungua kwa mvua baadaye mwezi huu, Wakenya wamehimizwa kuwa waangalifu kutokana na mvua inayoendelea kwa sasa ambayo bado inaweza kusababisha mafuriko, maji kusimama na kuvurugika kwa usafiri.

Idara ya hali ya hewa pia imeonya kuhusu hatari za kiafya zinazoweza kujitokeza kutokana na hali ya unyevunyevu, ikiwa ni pamoja na magonjwa yanayosababishwa na maji chafu na malaria, hasa katika maeneo yenye maboma duni ya maji taka.

Aidha, mvua inayoendelea katika maeneo ya Kati, Magharibi, Bonde la Ziwa Victoria na sehemu za Bonde la Ufa inaweza kusababisha maji kujaa mashambani na hivyo kuharibu mazao.

Katika maeneo ya Ukanda wa Kusini Mashariki, mvua ya wastani hadi chini ya wastani pamoja na vipindi vya dhoruba kali vinaweza kusababisha unyevu wa udongo kutokuwa sawa, hali inayoweza kudhoofisha mazao.

Idara hiyo pia imeonya kuwa mito, mabwawa na mifumo ya mifereji inaweza kujaa kupita kiasi kutokana na maji mengi, hali inayoongeza hatari ya mafuriko ya ghafla na mito kufurika, hasa katika maeneo ya tambarare na ya chini.