Makala

Sababu za Seneti kupendekeza sheria mpya ya uajiri katika kaunti

Na NDUBI MOTURI, BENSON MATHEKA May 2nd, 2026 Kusoma ni dakika: 2

KAMATI ya Seneti inapendekeza mabadiliko makubwa kuhusu jinsi kaunti zinavyoajiri wafanyakazi, ikiwemo kuruhusu watumishi kuhama kati ya kaunti mbalimbali hatua inayoweza kubadili pakubwa mfumo wa ajira katika serikali za ugatuzi.

Pendekezo hilo, lililotolewa na Seneta wa Marsabit Mohamed Chute, mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Seneti kuhusu Uwiano wa Kitaifa, Fursa Sawa na Ujumuishaji wa Kanda, linataka kurekebishwa kwa Sheria ya Serikali za Kaunti ili kushughulikia ukabila uliokithiri katika ajira za kaunti.

Bw Chute alisema kuwa kaunti nyingi huajiri wafanyakazi kutoka jamii zinazoishi eneo husika, mara nyingi kwa misingi ya ukabila na koo.

“Leo hii, katika kaunti nyingi, ajira nyingi hutolewa kwa jamii moja tu,” alisema, akieleza kuwa tatizo hilo limeenea katika kaunti zote 47.

Alikuwa akizungumza wakati wa kikao cha kamati hiyo kilichochunguza utaratibu wa ajira katika Bunge la Kaunti ya Garissa, ambapo Spika Abdi Idle na karani wa bunge hilo walihojiwa kuhusu madai ya ubaguzi wa koo katika ajira.

Maseneta walisema tatizo hilo si la Garissa pekee, bali linaonekana kote nchini, huku ripoti ya kamati hiyo ikionyesha kuwa ajira nyingi za kaunti zinaendea jamii moja.

Kwa mfano, kaunti ya Bomet ina asilimia 97.28 ya wafanyakazi kutoka jamii ya Kipsigis, Homa Bay ina asilimia 96.98 ya Waluo, Samburu asilimia 96.65 ya Wasamburu, na Elgeyo-Marakwet asilimia 96.22 ya Wakalenjin. Kaunti za Kirinyaga, Nyandarua na Nyeri pia zina idadi kubwa ya Wakenya kutoka jamii moja.

Ili kukabiliana na hali hiyo, kamati inapendekeza mfumo mmoja wa kuajiri, sawa na ule wa Tume ya Huduma ya Umma, ambao utaajiri wafanyakazi kwa niaba ya kaunti zote.

Lengo kuu ni kuunda tume ya kitaifa ya watumishi wa umma watakaosambazwa katika kaunti mbalimbali ili kuhakikisha usawa wa kikabila na kupunguza upendeleo wa wenyeji.

“Iwapo tunataka kufuata sheria ilivyo sasa, basi tunahitaji taasisi itakayoratibu ajira na uhamisho wa wafanyakazi katika kaunti zote 47,” alisema Bw Chute.

Pendekezo hilo pia linataka kushughulikia ubaguzi wa ndani ya jamii, hasa katika maeneo ya Kaskazini Mashariki ambako ajira hudhibitiwa na koo kubwa, na kuacha koo ndogo nje ya mfumo.

Hata hivyo, mabadiliko hayo yatahitaji kuvunjwa kwa baadhi ya vipengele muhimu vya mfumo wa sasa wa ajira za kaunti. Sheria ya sasa inaweka bodi za ajira za kaunti zinazojitegemea kusimamia uajiri katika mihimili ya bunge na serikali.

Marekebisho yanayopendekezwa yanalenga kufuta bodi hizo na kuanzisha chombo kimoja cha kitaifa kitakachosimamia ajira za kaunti zote.

Kwa mujibu wa Katiba ya Kenya ya 2010, kila kaunti inapaswa kuwa na huduma yake ya umma inayojitegemea, jambo ambalo maseneta sasa wanasema limechangia ukosefu wa uwiano wa kikabila.

“Kaunti nyingi zina zaidi ya asilimia 70 ya wafanyakazi kutoka jamii moja,” alisema Bw Chute.

Hata hivyo, pendekezo hilo linaibua maswali kuhusu mustakabali wa ugatuzi, kwani kuhamisha mamlaka ya ajira hadi kiwango cha kitaifa kunaweza kukabiliwa na upinzani kutoka kwa serikali za kaunti.