Habari

Mwanamke aliyekuwa na Dkt Obwaka kabla ya kifo chake kuzuiliwa siku 10

Na RICHARD MUNGUTI May 4th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

MAHAKAMA imeruhusu polisi kumzuilia kwa siku 10 mshukiwa anayehusishwa na kifo cha aliyekuwa mwenyekiti wa Bodi ya Hospitali ya Nairobi, Dkt Job Lukuru Obwaka, kilichotokea Mei 1, 2026.

Hakimu wa Mahakama ya Kibera aliamuru mshukiwa huyo, Beatrice Wangari, azuiliwe katika Kituo cha Polisi cha Kilimani ili kuruhusu maafisa kutoka Idara ya Upelelezi Nchini (DCI) kukamilisha uchunguzi na kukusanya ushahidi.

Mahakama ilifahamishwa kuwa mshukiwa anachunguzwa kwa kosa la mauaji.

“Mtuhumiwa aliyekamatwa kufuatia kifo cha Dkt Obwaka anachunguzwa kwa kosa la mauaji kinyume cha sheria,” akasema afisa cheo cha sajini Rhoda Nzioka kutoka DCI.

Katika ombi lake, Bi Nzioka aliomba mahakama iwaruhusu polisi kumzuilia mshukiwa kwa siku 14, ombi lililopingwa na wakili wake Levi Munyeri, ambaye aliomba mteja wake aachiliwe kwa dhamana akisema kuwa hana nia ya kutoroka.

Bw Munyeri aliiomba mahakama izingatie kuwa marehemu alipata matatizo ya kiafya alipokuwa nyumbani kwa mshukiwa huko Kitengela, na kwamba mshukiwa alifanya kila juhudi kumuokoa.

“Mteja wangu alimuita jirani alipoona marehemu ana tatizo la kiafya, akampigia simu daktari wake binafsi na kuomba ambulansi impeleke Hospitali ya Nairobi,” akaambia mahakama.

Wakili huyo aliongeza kuwa Dkt Obwaka alifariki dunia alipokuwa akipelekwa hospitalini na si katika nyumba ya mshukiwa.

Aliomba muda wa kuzuiliwa upunguzwe akisema mshukiwa hataingilia uchunguzi na kuuvuruga.

Kwa mujibu wa wa polisi, marehemu alimtembelea mshukiwa Mei 1, 2026 katika makazi yake ya Kitengela, ambapo inadaiwa aliandaliwa chakula.

“Dkt Obwaka aliendesha gari lake kutoka Nairobi hadi nyumbani kwa mshukiwa katika eneo la Milimani, Kitengela, Kaunti ya Kajiado, saa nane mchana,” ikasema maelezo ya polisi.