Siasa

Linda Mwananchi wamshambulia Ruto kwa hotuba anayopanga kutoa kwa Bunge la Tanzania

Na CECIL ODONGO May 5th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

VIONGOZI wanaogemea mrengo wa Linda Mwananchi jana walimkosoa vikali Rais William Ruto kufuatia hotuba anayotarajiwa kutoa katika Bunge la Tanzania Jumanne, Mei 5, 2026.

Walisema hotuba hiyo haina maana na haifai ikizingatiwa kile walichokitaja kuwa kuzorota kwa haki za binadamu nchini humo.

Rais Ruto anatarajiwa kutoa hotuba ya kihistoria katika Bunge la Tanzania, ambapo anatazamiwa kuzungumzia uhusiano unaokua kati ya Kenya na Tanzania pamoja na changamoto zinazoikumba Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Hakuna Rais wa Kenya aliye madarakani ambaye amewahi kuhutubia Bunge la Tanzania tangu nchi hiyo ipate uhuru mnamo 1961.

Rais mstaafu wa Tanzania Jakaya Kikwete naye aliwahutubia wabunge wa Bunge la Kitaifa na Seneti hapa nchini mnamo Oktoba 6, 2015.

Bw Kikwete aliwavutia wengi kutokana na ufasaha wake katika lugha ya Kiswahili baada ya kutoa hotuba yake kwa Kiingereza.

Katika taarifa, Linda Mwananchi, ambao ni mrengo wa ODM unaoegemea upande wa Katibu Mkuu Edwin Sifuna, ilidai kuwa Kenya na Tanzania zinaendelea kukandamiza demokrasia na utawala wa sheria, na hivyo hotuba ya Rais Ruto haina umuhimu kwa wananchi wa mataifa hayo mawili.

“Matukio ya hivi karibuni nchini Tanzania yanaifanya hotuba hii kuwa usaliti si tu kwa wananchi wa Tanzania bali pia kwa misingi ya demokrasia na uhuru ambayo Wakenya wanathamini,” ilisema taarifa hiyo.

Taarifa hiyo ilitiwa saini na viongozi 16 akiwemo Gavana wa Siaya James Orengo, Seneta wa Vihiga Godfrey Osotsi, Katibu Mkuu wa ODM Edwin Sifuna na Mbunge wa Embakasi Mashariki Babu Owino.

“Tunalazimika kuzungumza kwa sababu urais wa Kenya ni ishara ya mamlaka ya taifa letu, na mwenye kiti hicho hapaswi kuitumia kwa matakwa yake binafsi,” wakaongeza.

Kundi hilo pia lilikosoa utawala wa Rais wa Tanzania Samia Suluhu Hassan, likirejelea uchaguzi mkuu wa Oktoba mwaka jana ambao walisema haukufikia viwango vya uchaguzi huru na wa haki.

Rais Samia alitangazwa mshindi kwa asilimia 98 ya kura na Tume ya Uchaguzi ya Tanzania Novemba 1.

Matokeo hayo yalisababisha maandamano makubwa yaliyosababisha uharibifu wa mali. Kiongozi wa upinzani Tundu Lissu alizuiwa kushiriki uchaguzi huo na bado anazuiliwa, huku pia kukiwa na madai ya kunyanyaswa kwa viongozi wengine wa upinzani.

Mnamo Aprili 23, Tume ya uchunguzi iliyoongozwa na Jaji Mkuu mstaafu Mohamed Chande Othman iliripoti kuwa watu 518 waliuawa wakati wa maandamano hayo.

“Tunaweza kusema kwa uhakika kuwa viwango vya demokrasia na haki havikufikiwa, hasa ikizingatiwa kuwa wawakilishi wa upinzani walizuiliwa,” iliongeza taarifa hiyo.

“Kwa kuhutubia Bunge la Tanzania, Rais Ruto anaweza kuonekana kuhalalisha utawala na mchakato wa uchaguzi ambao si huru na haki.”