Habari

Uhasama watokota tena kati ya DCP na Jubilee kuhusu Ol Kalou

Na MWANGI MUIRURI May 11th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

UHASAMA wa kisiasa unazidi kutokota kati ya Jubilee na DCP baada ya vyama hivyo viwili kusema vitakuwa na mgombeaji kwenye uchaguzi mdogo wa Ol Kalou.

Baada ya DCP kuandaa mchujo wake, sasa ni dhahiri kuwa chama hicho kitakuwa na mgombeaji na hakutakuwa na ushirikiano wa kisiasa upinzani jinsi ilivyokuwa katika kura ya Mbeere Kaskazini mnamo Novemba mwaka jana.

Aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua analenga kutumia uchaguzi huo mdogo kuonyesha kuwa ndiye kigogo wa siasa za Mlima Kenya.

Kwa upande mwingine Rais Mstaafu Uhuru Kenyatta ambaye ni kiongozi wa Jubilee, ametangaza kuwa anamuunga mkono Dkt Fred Matiangí kwa urais mnamo 2027 na analenga kudhihirisha kuwa licha ya kuondoka mamlakani, bado ana ushawishi kisiasa eneo la Mlima Kenya.

Kwa mujibu wa mbunge wa zamani wa Starehe Maina Kamanda, Jubilee lazima ijifunze kuwa upinzani utaendelea kuungana tu iwapo mbinu za kushinda viti zitakumbatiwa badala ya ubabe wa kisiasa.

“Sisi ni miungano ya vyama mbalimbali na lazima tujue kuwa ngome ya kila chama ndiyo itaamue unapata nini kwenye muafaka wa upinzani,” akasema.

Bw Kamanda ambaye pia ni Mwenyekiti wa Baraza la Viongozi wakongwe wa kutoa ushauri ndani ya DCP.

Alimtaka Dkt Matiangí amakinikie kuunganisha ngome yake ya Gusii badala ya kushinda na DCP Mlimani.

“Mnamo 20022, marehemu Simeon Nyachache alichukua chama cha Ford People ambacho kilikuwa na asili yake Mlima Kenya kutoka kwa Kimani wa Nyoike na kukifanya kuwa maarufu Gusii. Dkt Matiangí anastahili kufuata mkondo huo na kuhakikisha Jubilee inajizolea umaarufu wake Gusii,” akasema Bw Kamanda.