Habari

Watoto wengi wa Onyonka wazua gumzo mazishini Kisii

Na RUTH MBULA May 18th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

SENETA wa Kaunti ya Kisii, Richard Momoina Onyonka, aliwaacha maelfu wakiwa wamepigwa na butwaa alipojitambulisha kama baba wa wengi katika mazishi ya mama yake, Teresia Omoke.

Idadi kubwa ya watoto waliotambulishwa kama wajukuu wa marehemu, zaidi ya nusu walikuwa wake.

Sehemu kubwa ya watoto ni wavulana wenye maumbile yanayofanana na seneta huyo.

Anakiri kuwa na wake zaidi ya watano.

Ajabu ni kuwa, hakuna yeyote miongoni mwa wake zake wengi aliyetambulishwa, isipokuwa tu Dkt Roselyn Akombe, anayefanya kazi katika Umoja wa Mataifa, New York.

Bi Akombe, kamishna wa zamani wa Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) alizungumza katika mazishi ya mama yake Richard akisema alikuwa mama mzuri kwa wote.

“Aliwalinda sana watoto wake. Nilitumia muda mwingi naye, na usiniulize vipi. Lakini nilitumia muda mwingi na mama kwa sababu ya mjukuu aliyezungumza awali…nataka kuwahimiza wajukuu wa mama Teresia’ kwa sababu alipenda elimu, waanzishe ufadhili, kwa jina la Mama Teresia.

Naanza kwa kuweka Sh 200, 000,” alisema Bi Akombe.

Idadi kubwa ya watoto hao, kuanzia na bintiye mkubwa, Moraa, walizaliwa na kina mama tofauti wanaoishi Amerika.

Mwakilishi Mwanamke Kisumu, Ruth Odinga alizidisha kisanga cha “mabibi” zake wengi alipotangaza kwenye mazishi hayo kuwa yeye vilevile aliwahi kuwa mpenziwe Richard,alipokuwa mwanafunzi katika Shule ya Upili ya Asumbi Girls akiwa katika Shule ya Upili ya Kisii miaka ya 1970.

“Richard, mnavyomsikia akiitwa Momoima… wacha niseme tu… Momoima, nimeona una watoto wengi kote… Momoima ako na wamama pia… lakini mliyeanza naye maisha nikiwa msichana mdogo katikaAsumbi Girls, na ukiwa Kisii Boys… si mwingine ila Ruth Odinga,” alisema Bi Odinga, akizua kicheko miongoni mwa waombolezaji.

Seneta Onyonka alichaguliwa kuwakilisha eneobunge la Kitutu Chache 2007 baada ya kumbwaga mshindani wa marehemu baba yake, Jimmy Angwenyi.
Aliteuliwa mara moja kama naibu waziri wa masuala ya kigeni na ushirikiano kimataifa ambapo alihudumu miaka mitano.

Richard alienda Amerika katika miaka ya 1980 ambapo baba yake, Dkt Onyonka, alihudhuria ndoa iliyofanyika New Jersey.

Nyumbani kwake kijijini, anaishi na mke wake anayefahamika kama Beatrice Gesare, anayemwakilisha katika shughuli mbalimbali Kisii.

Aliondoka Amerika 1992 kurejea nyumbani kusaidia kumfanyia kampeni baba yake ambaye afya yake ilizorota baada ya kuugua kiharusi.

Maisha yake akiwa mchanga yalizingirwa na utata sawia na muundo wa familia yake sasa.

Alizaliwa miaka ya 1960 kabla ya baba yake kuhamia Amerika kusoma na kumwacha nyuma na mama yake.

Kutokana na shaka kuhusu baba yake kurejea, mama yake aliolewa tena na mwalimu wa shule ya msingi, Joseph Omoke, aliyempokea na kumlea Richard hadi alipokamilisha Kidato cha Nne ambapo Dkt Onyonka alikuja kumwitisha.

Dkt Onyonka alipomtwaa Richard, alikuwa na familia thabiti.

Richard alilelewa na baba wawili katika boma mbili tofauti katika sehemu mbili tofauti maishani mwake.