Kindiki: Ruto ameitisha mkutano saa kumi jioni kuangalia vile tutapunguza bei ya mafuta
NAIBU Rais Kithure Kindiki amesema amefanya mkutano mtandaoni na Rais William Ruto ambapo wamejadili suala la mgomo wa wahudumu wa uchukuzi ambao umesababisha shughuli za usafiri kukwama kote nchini.
Prof Kindiki amesema haya wakati wa mkutano na viongozi wa Tharaka uliofanyika nyumbani kwake, Irunduni, Kaunti ya Tharaka Nithi. Rais Ruto yumo ziarani nchini Azerbaijan alikoenda kwa kongamano kuhusu makazi ya mijini, ambapo serikali ya Kenya ilitarajiwa kuzungumzia ufanisi wa mradi wa makazi nafuu, maarufu kama Affordable Housing Program.
Mgomo wa wahudumu wa uchukuzi ulioanza kutekelezwa saa sita usiku wa kuamkia Jumatatu, Mei 18, 2026, umelemaza uchukuzi na biashara katika miji mingi huku Nairobi, Kitengela, Meru, Kisii, Murang’a, Machakos, Kitale ikiwa miongoni mwa iliyoathirika zaidi.
Kufikia saa kumi jioni, usafiri bado ulikuwa wa shida katika maeneo mengi huku magari machache yaliyoonekana barabarani yakipigwa mawe na vijana au kushurutishwa kuondoka.
Katika miji ya Ruiru, Kasarani na Juja, Nairobi, polisi walikuwa na wakati mgumu kukabiliana na makundi ya wakazi walioanza kuimba nyimbo za kukashifu serikali.
Polisi walilazimika kurusha vitoa machozi kutawanya waandamanaji huku hali ikiendelea kuwa ya taharuki.
Taarifa zaidi ni kadiri tunavyozipokea…