Makala

Mgomo wa matatu: Thika Road yasalia mahame

Na SAMMY WAWERU May 18th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

BARABARA kuu Kenya – inayounganisha jiji la Nairobi na mji wa Thika, Jumatatu asubuhi Mei 18, 2026 ilisalia kufungwa kufuatia mgomo wa matatu dhidi ya bei ya mafuta ya petroli uliotekelezwa maeneo tofauti ya nchi.

Wamiliki wa matatu, wahudumu, magari ya kibinafsi, teksi na wana bodaboda walisitisha shughuli za uchukuzi wa umma na usafiri, wakitaka bei ya mafuta ya petroli ishushwe.

Aidha, wanapinga bei ya juu ambapo Mamlaka ya Kudhibiti Kawi na Petroli (EPRA) mnamo Alhamisi, Mei 14, 2026 ilitathmini bei itakayotumika kati ya Mei hadi Juni 14. EPRA iliongeza bei ya dizeli kwa Sh46.29 kwa lita, huku bei ya petroli ikiongezeka kwa Sh16.65 kwa lita. Hivyo basi, petroli sasa inauzwa Sh214.25 kwa lita na dizeli kwa Sh242.92, huku bei ya mafuta ya taa ikisalia Sh152.78.

Gari Thika Super Highway likitumia leni isiyofaa kwa hofu ya kuvamiwa na waandamanaji. Picha|Sammy Waweru

Huku sehemu nyingi za taifa haswa mijini uchukuzi wa umma ukisimamishwa, Thika Super Highway, kati ya asubuhi hadi adhuhuri, mnamo Jumatatu, barabara hiyo kuu ilisalia mahame.

Ikiwa ni njia yenye shughuli tele za uchukuzi wa umma na usafiri, barabara hiyo kuu Kenya iliyoundwa na Rais mstaafu marehemu Mwai Kibaki, ni magari machache mno yaliyoonekana yakipita.

Majira ya saa tatu na nusu hivi asubuhi (9:30am), makarandinga ya polisi yalionekana yakipita kwa kasi kuelekea Githurai 45 na Ruiru, ambapo ilikuwa imefungwa na waandamanaji.

Cha kushangaza, baadhi ya magari yalionekana kufanya abautani – yakitumia leni isiyofaa kwa hofu ya kushambuliwa. Kulingana na wahudumu wa matatu, bei ya EPRA inalemaza biashara – hatua ambayo imewalazimisha kuongeza nauli mara dufu.

Karandinga ya polisi Thika Road ikielekea Githurai 45 na Ruiru kufungua barabara iliyofungwa. Picha|Sammy Waweru

Mwenyekiti wa kitaifa wa Chama cha Wamiliki wa Matatu, Albert Karakacha, alidokeza kuwa mgomo huo wa Jumatatu ulifanikiwa kwa asilimia 99, na kwamba Wakenya wanapaswa kutarajia hali hiyo hiyo kuendelea hadi Jumanne. “Hilo litaendelea hadi wakati serikali itakapokubali kuketi nasi mezani kwa mazungumzo na wadau husika mafuta ya petroli yashuke.”

Maafisa wa polisi wa kawaida na wale wa kukabiliana na ghasia, mchana kutwa walikabiliana vikali na waandamanaji waliofunga barabara Jijini Nairobi, Nakuru, Kisii, Machakos, Makueni, na miji mingine. Magurudumu yaliwashwa moto na waandamanaji, wakionyesha ghadhabu zao dhidi ya bei ya juu ya mafuta ya petroli. Serikali, hata hivyo, imeendelea kutetea bei ya EPRA ikisema mfumko huo unasababishwa na vita vinavyoendelea kati ya Iran na Israili.